Aug 02, 2021 03:16 UTC
  • Kuzinduliwa maabara ya kwanza ya bioteklolojia ya isotopu; mafanikio mengine katika uwanja wa matibabu ya nyuklia nchini Iran

Hii leo, elimu ya udaktari na utabibu ina uhusiano wa karibu sana na teknolojia ya nyuklia kiasi kwamba nchi zilizoendelea kiviwanda zinatumia pakubwa tekniolojia hiyo katika nyanja za sayansi ya udaktari na matibabu.

Katika kukidhi mahitaji hayo muhimu ya kisayansi, Jumamosi iliyopita  maabara ya kwanza ya bioteknolojia ya isotopu ilizinduliwa katika Kituo cha Maji Mazito cha Arak.Vile vile jiwe la msingi liliwekwa kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha Maabara za Kimia kwa lengo la kunufaika na maji mazito. Kituo hicho kitajengwa kwa lengo la kuzuia kuuzwa nje ya nchi malighafi ya maji hayo na kwa ajili ya kukidhi mahitaji ya sekta ya tiba na vipimo vya kidaktari nchini.

Akizungumza katika sherehe za uzinduzi wa mradi huo muhimu wa utafiti na uzalishaji, Ali Akbar Salehi, Mkuu wa Shirika la Nishati ya Atomiki la Iran alisema kuwa mradi huo ni nembo ya uwezo wenye thamani kubwa wa taifa la Iran na kuongeza kwa kusema: Mradi huu mkubwa ambao unajumuisha utafiti na uzalishji katika sekta ya teknolojia umepatikana kutokana na juhudi za pamoja za familia ya Shirika la Nishati ya Atomiki la Iran na sekta ya Afya nchini, na utafanikishwa pakubwa na teknolojia ya nyuklia.

Maabara hiyo inatazamiwa kutumia isotopu kwa ajili ya kutambua mapema maradhi ya saratani pamoja na kuzalisha vifaa na zana za kitiba kwa ajili ya matumizi ya madaktari. Mbinu hiyo ilianza kutumika duniani mwaka 2019, nayo Iran imekuwa ikienda sambamba na mafanikio hayo ya kimataifa. Isotopu zina matumizi mengi na muhimu ya kielimu ambayo huwekwa katika viwango tofauti na maalumu vya fizikia, kemia na nyuklia.

Ali Akbar Salehi, Mkuu wa Shirika la Nishati ya Atomiki la Iran

Katika kunufaika na teknolojia ya nyuklia, Jamhuri ya Kiislamu ya Iran inafungamana kikamilifi ma maazimio pamoja na sheria za kimataifa katika uwanja huo na imeweza kufikia mafanikio makubwa katika sekta ya teknolojia ya nyuklia kwa kushirikiana na kuwaruhusu wakaguzi wa Wakala wa Kimataifa wa Nishati ya Nyuklia IAEA kukagua mara kwa mara vituo vyake vya nyuklia.

Ayatullah Ali Khamenei, Kiongozi Maudhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu, amesisitiza mara nyingi juu ya umuhimu wa nchi hii kunufaika na teknolojia ya nyuklia na kuongeza kuwa Iran haitaki hata kidogo kutumia teknolojia hiyo katika utengenezaji wa silaha za nyuklia.

Akizungumza huko nyuma mbele ya hadhara ya wasomi na Wairani wenye vipawa maalumu vya kieleimu, Ayatullah Khamenei alisema: Ikiwa elimu itatenganishwa na utamaduni ulio sahihi, bila shaka elimu hiyo itapotosha. Kutofungamanishwa elimu ya nyuklia yenye manufaa na utamaduni unaojali maslahi ya mwanadamu, kulisababisha kuundwa bomu la nyuklia na hii leo pia hilo bado ni tishio. Sisi pamoja na kuwa tumekuwa na uwezo wa kutengeneza bomu hilo lakini tumekuwa na uamuzi thabiti na wa kishujaa wa kutotembea kwenye njia hiyo. Kutengeneza bomu la nyukilia na pia umiliki wake ni makosa makubwa kwa sababu matumizi yake ni haramu."

Kutokana na matumizi yake mengi, teknolojia ya nyuklia ina umuhimu mkubwa katika ustawi wa elimu na bila shaka ni moja ya misingi muhimu katika ustawi endelevu na pia katika mambo ya msingi yanayoifanya nchi kuendelea na kuwa na uwezo mkubwa katika nyanja tofauti. Ni kutokana na ukweli huo ndipo sayansi na teknolojia ya nyuklia ikawekwa kwenye kiwango cha teknolojia bora na zilizoendelea ulimwenguni.

Nchini Iran pia kuna maendeleo makubwa ambayo yamepatikana katika sekta ya teknolojia mpya za nyuklia, na licha ya kuwepo vikwazo vya kidhalimu na mashinikizo ya kiwango cha juu kabisa ya Marekani, lakini watafiti na wasomi wake wamefanikiwa katika miaka ya karibuni kufikia maendeleo makubwa ya kinyuklia na hivyo kuweza kutengeneza vifaa na dawa zinazotokana na sayansi ya nyuklia kwa ajili ya kugundua na kutibu magonjwa tofauti sugu yakiwemo ya saratani.

Makao makuu ya Shirika la IAEA mjini Vienna Austria

Kuhusu hatua zilizochukuliwa na Shirika la Nishati ya Atomiki la Iran katika kutekeleza sheria iliyopitishwa na Majlisi ya Ushauri ya Kiislamu ya Iran (bunge) kwa ajili ya kulinda haki za nyuklia za taifa hili, Behrouz Kamalvandi, msemaji wa shirika hilo anasema: Urutubishaji urani kwa kiwango cha asilimia 20 na 60, ujenzi wa tanuri jipya la maji mazito, uwekaji wa mashinepewa mpya na za kisasa na uzinduzi wa kiwanda kipya cha urutubishaji urani ya chuma cha pua ni baadhi tu ya hatua  muhimu zilizochukuliwa katika uwanja huo.

Maendeleo hayo yanathibitisha wazi kuwa hata kama nchi za Ulaya zilikiuka ahadi na kuamua kutoshirikiana na Iran katika utekelezaji wa mpango wake wa nyuklia wenye malengo ya amani, lakini wataalamu na wanasayansi wa nyuklia wa Iran wamefanikiwa pakubwa kuondoa vizuizi njiani na kuliletea taifa mafanikio makubwa katika sekta ya tejnolojia ya nyuklia.

Hii leo Iran ina ujuzi na uwezo mkubwa katika nyanja za miundomsingi ya sayansi ya nyuklia kwa kutegemea utaalamu wa ndani ya nchi na sasa imekuwa marejeo muhimu ya kielimu katika uwanja huo. Kwa msingi huo, iko tayari kuzipa nchi nyingine za dunia elimu na uzoefu wake katika uwanja wa matumizi salama na ya amani ya nyuklia, yakiwemo matumizi ya tiba na matibabu.