Aug 03, 2021 14:34 UTC
  • Raeisi: Tunataka kuondolewa vikwazo lakini hatutegemea madola ya kigeni

Rais mpya wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema kuwa serikali yake inataka kuondolewa vikwazo haramu vilivyowekwa na madola ya kibeberu dhidi ya Iran lakini suala hilo halitafungamanishwa na matakwa ya madola ajinabi.

Rais Sayyid Erahim Raeisi ameyasema hayo leo katika sherehe ya kuidhinishwa rasmi kuwa Rais wa Serikali ya 13 ya Iran na kuongeza kuwa: Kuzingatiwa maagizo ya Imam Ruhullah Khomeini na miongozo ya Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu kumepelekea kupatikana maendeelo na ustawi hapa nchini.

Rais Sayyid Raeisi amesema: Jua angavu la demokrasia ya kidini lilichomoja katika ardhi hii zaidi ya miaka 40 iliyopita chini ya uongozi wa hayati Imam Khomeini na hima kubwa ya wananchi wanaojua vyema majukumu yao wa Iran.

Rais mpya wa Iran amesema kuwa, katika kipindi chote cha zaidi ya miaka 40 iliyopita viongozi wa serikali wamefanya jitihada kubwa za kuimarisha demokrasia ya kidini hapa nchini na kuongeza kuwa, kadiri maagizo ya Imam Khomeini na Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi yalivyotekelezwa ndivyo Iran ilivyopata maendeleo, uwezo na ustawi. 

Kiongozi Muadhamu akimuidhinisha rasmi Raeisi kuwa rais mpya wa Iran

Amesema Jamhuri ya Kiislamu imeonesha mfumo mpya wa utawala duniani ambao umeunganisha pamoja dini na dunia, maadili na maendeleo na izza na hali bora ya maisha.

Rais mpya wa Iran amesema serikali yake itaanza kushughulikia matatizo ya nakisi ya bajeti, uthabiti wa soko la hisa, kudhibiti mfumuko wa bei, maambukizi ya corona na masuala mengine kadhaa. 

Amesisitiza kuwa Jamhuri ya Kiislamu inataka kuondolewa vikwazo lakini hali ya maisha ya wananchi haitafungamanishwa na siasa za madola ya kibeberu. 

Sayyid Ibrahim Raisi ambaye alishinda uchaguzi mkuu uliopita wa rais ameidhinishwa rasmi leo na Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu kuwa rais mpya wa serikali ya 13 ya Jamhuri ya Kiislamu.

Katika hati ya kuidhinishwa serikali hiyo mpya, Kiongozi Muadhamu amesisitiza udharura wa kupewa nafasi tabaka la vijana serikalini, kuondolewa vikwazo vinavyozuia uzalishaji, kuimarishwa thamani ya sarafu ya taifa na kutatuliwa matatizo ya wananchi pamoja na kuwezeshwa katika nyanja tofauti.