Wairani waanza safari ya kulekea ardhi ya Wahy kwa ajili ya ibada ya Hija
Misafara ya kwanza ya Wairani wanaoelekea katika ardhi ya wahyi kwa ajili ya ibada ya Hija imeondoka nchini mapema leo.
Kwa mujibu wa Shirika la Habari la IRIB, misafara ya kwanza ya Wairani wanaolekea Hija imeondoka katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Imam Khomeini (RA) jijini Tehran leo asubuhi kuelekea Ardhi ya Wahyi.
Hujjat al-Islam Syed Abdul Fattah Nawab, mwakilishi wa Faqihi Mtawala katika masuala ya Hijja na Ziyara ambaye pia ni msimamizi wa Mahujaji wa Iran ameuaga msafara huo na kusema: "Kauli mbiu ya Hija ya mwaka huu ni "Uzingatiaji Qur'ani, Huruma na Nguvu za Kiislamu na Kutetea Palestina Inayodhulumiwa." Amewashauri wanaoelekea Hija kuwa, wanapotembelea Al Masjid An Nabawi (SAW ) na Masjid Al-Haram wajitahidi kuhitimisha qiraa ya Qur'ani Tukufu.
Msimamizi wa Mahujaji wa Iran aidha amesema nguvu na uwezo wa Kiislamu na Palestina inayodhulumiwa ni sehemu nyingine ya nara ya Hija ya mwaka huu. Ameongeza kuwa Mahujaji wanapaswa kufuata sira ya Manabii na kuwaombea ushindi wananchi wa Palestina wakiwa katika ardhi ya Wahyi.
Kila mwaka katika mwezi wa Dhul Hijjah, Saudi Arabia hukaribisha Waislamu wapatao milioni mbili wanaonuia kutekeleza ibada ya Hijja. Mwaka huu, Mahujaji 87,550 wa Iran wanatazamiwa kufika katika ardhi ya Wahyi kuhiji.