Maelfu ya Wairaqi wajiandikisha kuingia vitani kuisaidia Iran endapo itashambuliwa na Marekani
https://parstoday.ir/sw/news/west_asia-i136386-maelfu_ya_wairaqi_wajiandikisha_kuingia_vitani_kuisaidia_iran_endapo_itashambuliwa_na_marekani
Maelfu ya Wairaqi wamesaini hati ya ahadi ya kusaidia kuihami Jamhuri ya Kiislamu ya Iran iwapo itashambuliwa kijeshi na Marekani.
(last modified 2026-03-03T16:16:59+00:00 )
Feb 08, 2026 06:16 UTC
  • Maelfu ya Wairaqi wajiandikisha kuingia vitani kuisaidia Iran endapo itashambuliwa na Marekani

Maelfu ya Wairaqi wamesaini hati ya ahadi ya kusaidia kuihami Jamhuri ya Kiislamu ya Iran iwapo itashambuliwa kijeshi na Marekani.

Kwa mujibu wa taarifa, karibu watu 5,000 katika jimbo la Diyala nchini Iraq walikusanyika kutangaza nia yao ya kuihami Iraq na jirani yake wa mashariki yaani Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, pamoja na makundi ya Muqawama yanayoungwa mkono na Iran, "bila ya kuhitaji kufidiwa chochote".

"Tunatangaza utayari wetu wa kujitolea kusaidia vikosi vyetu vya usalama, Vikosi vya Kujitolea vya Wananchi, na Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, na tunapinga waziwazi uingiliaji wa Marekani katika Jamhuri ya Kiislamu," taarifa hiyo imesema.

Ammar al-Tamimi, kiongozi wa harakati ya Muqawama wa Badr ambayo ndiyo iliyoratibu mkusanyiko wa wapiganaji wa kujitolea huko Diyala, amesema, wapiganaji hao hawana uhusiano na kundi lolote maalumu la Muqawama.

"Sisi zaidi ni watu wa kujitolea walio tayari kuhudumu kama kikosi cha akiba kwa ajili ya vikosi vya usalama," ameeleza Tamimi katika mahojiano na tovuti ya habari ya Rudaw.

Kuhusiana na wapiganaji hao wa kujitolea, kiongozi huyo wa harakati ya Badr amesema: "mjumuiko huu una majina 4,947; na muundo wake wa kitaasisi, pamoja na jina la kila mpiganaji wa kujitolea, vitawasilishwa kwa Kamandi ya Operesheni ya Diyala, ambayo itavipeleka kwa Kamanda Mkuu wa Vikosi vya Ulinzi."

Makundi ya Muqawama ya Iraq yanayoungwa mkono na Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, yakiwemo ya Kataeb Hezbollah na Harakat al-Nujaba nayo pia yameanzisha vituo vya uandikishaji kote nchini Iraq, ikiwemo katika mji mkuu Baghdad, ili kusajili wapiganaji wa kujitolea watakaoingia vitani endapo Marekani itaishambulia kijeshi Iran.../