Balozi Saffar: Iran na Uganda kuendeleza uhusiano wao mzuri baina yao
Balozi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran mjini Kampala Uganda amesema kuwa, kifo cha Rais Ebrahim Raisi hakitaathiri uhusiano mzuri uliopo baina ya mataifa hayo mawili.
Balozi Majid Saffar ametoa hakikisho hilo katika mazungumzo yake na Rais Yoweri Museveni wa Uganda aliyekwenda katika ubalozi wa Iran mjini Kampala kwa ajili ya kutoa mkono wa pole kufuatia kifo cha Rais Ebrahim Raisi, waziri wake wa mambo wan je na maafisa wengine walioaga dunia siku ya Jumapili katika ajali ya helikopta.
Balozi wa Iran mjini Kampala amesisitiza kuwa, ushirikiano na uhusiano mzuri baiina ya Iran na Uganda utaendelea katika nyanja mbalimbali.
Aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran Ayatullah Ebrahim Raisi alizikwa jana katika Haram tukufu ya Imam Ridha (as) katika mji wa Mash'had huku mwili wa Hussein Amir-Abdollahian, aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ambaye naye alikufa shahidi katika ajali ya helikopta iliyotokea Jumapili iliyopita kaskazini magharibi mwa nchi ukizikwa jana pia katika Haram ya Shah Abdul-Adhim Hassani katika mji wa Rey, kusini mwa Tehran.
Mahudhurio makubwa ya wananchi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran katika shughuli ya mazishi ya shahidi Ebrahim Raisi na wenzake ambao walikufa shahidi katika ajali ya helikopta katika eneo la milimani la mkoa wa Azarbaijan Mashariki, kaskazini-magharibi mwa Iran kwa mara nyingine tena yamedhihirisha mshikamano na umoja wa taifa la Iran na nia yao ya kuendeleza njia ya mapambano na muqawama.