Ayatullah Kashani: Marekani imekasirishwa na ustawi wa Iran
Khatibu wa Sala ya Ijumaa iliyosaliwa leo hapa mjini Tehran amesema kuwa, Marekani imekasirishwa na ustawi wa kasi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na kuongeza kuwa: "Watawala wa Marekani watakufa kwa hasira zao".
Ayatullah Mohammad Imami Kashani katika hotuba zake za Sala ya Ijumaa amesisitiza kuhusu kumfahamu adui na njama zake na kuongeza kuwa: "Hatua ya Rais Donald Trump wa Marekani kujiondoa katika mapatano ya nyuklia ya Iran, maarufu kama JCPOA ni ishara kuwa, wakuu wa nchi hiyo wana tatizo na Uislamu na wanataka kutoa pigo kwa jamii za Kiislamu."
Ayatullah Imami Kashani amesema maadui wanataka kuona Umma wa Kiislamu daima ukiwa na matatizo ya kiuchumi na kiusalama na kuongeza kuwa: "Maadui wanafahamu fika kuwa, Uislamu ni chanzo cha kustawi, kupata nguvu na izaa jamii na hivyo daima huwa wanalenga kutoa pigo kwa dini hii tukufu ya Mwenyezi Mungu."
Khatibu wa Sala ya Ijumaa Tehran amebaini kuwa njia za kukabiliana na njama za maadui ni kumuamini Mwenyezi Mungu, kuwa imara, kutumia uwezo wa ndani ya nchi, umoja na mshikamano na kutumia nguuvu kazi ya vijana.
Ayatullah Imami Kashani amesema kwa yakini Umma wa Kiislamu duniani utakuwa na mustakabali mwema na maadui wataangamizwa.