Taasisi za Kiislamu zaonya kuhusu njama ya Marekani dhidi ya Nigeria
-
Taasisi za Kiislamu zaonya kuhusu njama ya Marekani dhidi ya Nigeria
Taasisi za Kiislamu nchini Nigeria zimetangaza kuwa, hatua ya tume ya kutafuta ukweli ya bunge la Marekani ya kuandaa ripoti ya upande mmoja kuhusu mizozo ya kikabila katika nchi hiyo ya Kiafrika ni ya kuzusha mifarakano.
Kulingana na ripoti ya Shirika la Habari la Mehr, ikinukuu The Guardian, Kongamano la Waislamu na Idara ya Maulama wa Kiislamu, mashirika mawili ya Kiislamu nchini Nigeria, yamekosoa katika taarifa tofauti ziara ya hivi karibuni ya ujumbe wa uchunguzi wa bunge la Marekani katika jimbo la Benue lenye wakazi wengi wa Kikristo, na kuielezea kuwa ya upendeleo na kinyume na kuishi kwa amani kwa wafuasi wa dini tofauti.
Katika taarifa tofauti, makundi hayo yalieleza kuwa ujumbe wa Marekani, uliotumwa kuchunguza madai ya mauaji ya Wakristo, ulikutana tu na viongozi wa Kikristo na mmoja wa machifu wa kikabila wa Benue, huku ukipuuza jamii za Waislamu na waathiriwa katika maeneo yenye Waislamu wengi.
Haji Abdul-Wasi Taiwo Bangbala, kiongozi wa Baraza la Waislamu la Nigeria, alisisitiza umuhimu wa ushirikiano wa kimataifa kuhusu changamoto za kiusalama za Nigeria, akisema kuwa, maingiliano hayo lazima yawe na msingi wa haki na uelewa kamili wa utofauti wa kidini na kijamii wa nchi hiyo.
Aliongeza kuwa kushindwa kwa ujumbe wa uchunguzi wa Bunge la Marekani kukutana na Baraza Kuu la Waislamu nchini Nigeria na taasisi nyingine muhimu za Kiislamu kunatia shaka uhalali wa dhamira ya ujumbe huo na kunaweza kuimarisha kauli za kufarakanisha.
Sehemu ya taarifa hiyo imeeleza: Changamoto tata za kiusalama za Nigeria haziwezi kuchanganuliwa kwa mtazamo wa dini moja. Kupunguza mashauriano kwa upande mmoja tu wa mzozo kunaweza kupotosha hadhira ya kimataifa na kuongeza mivutano ya ndani.