China yaionya Israel dhidi ya kuzuia makubaliano ya Iran na Marekani
-
Lin Jian
China imeionya Israel dhidi ya kuzuia utekelezaji wa Mkataba wa Maelewano (MoU) kati ya Iran na Marekani, huku ikitaka pande zote kuchukua hatua za vitendo kuunga mkono amani ya kikanda na kuunda mazingira yanayofaa kwa mazungumzo yajayo.
Beijing imekaribisha kutiwa saini kwa mkataba huo, ikithibitisha tena uungaji mkono wake kwa amani na uthabiti katika eneo la Asia Magharibi na Ghuba ya Uajemi.
Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya China, Lin Jian, ameionya Israel dhidi ya kudhoofisha utekelezaji wa makubaliano hayo wakati akijibu maswali kuhusu hatua ya kwanza ya makubaliano hayo na duru inayofuata ya mazungumzo kati ya Iran na Marekani.
Lin alisema: “Katika hatua hii nyeti, pande husika, ikiwemo Israel, zinapaswa kufuata mwelekeo mkuu wa amani na uthabiti katika eneo hili na kuchukua hatua za kusaidia Iran na Marekani kutekeleza makubaliano hayo pamoja na kuendeleza mazungumzo ya awamu ya pili, badala ya kufanya kinyume chake.”
Mwanadiplomasia huyo wa China pia amesisitiza umuhimu wa kimkakati wa uhusiano kati ya Beijing na Tehran, akizitaja nchi hizo mbili kuwa washirika wa muda mrefu wanaojitolea kuimarisha ushirikiano wao.
Amesema: “Kwa kuwa mshirika wa kimkakati wa kina wa Iran, China iko tayari kuimarisha na kuongeza imani ya kisiasa ya pande mbili na Iran, kupanua ushirikiano wenye manufaa ya pamoja katika nyanja mbalimbali, na kusukuma mbele zaidi ushirikiano wa kimkakati wa kina kati ya China na Iran."
Kauli za Beijing zinaakisi kuongezeka kwa uungwaji mkono wa kimataifa kwa Mkataba wa Maelewano kati ya Iran na Marekani, pamoja na upinzani dhidi ya juhudi zozote za utawala wa Israel za kuzuia utekelezaji wake.