Waziri Kiongozi wa Scotland: Uingereza inapaswa kusimamisha mauzo ya silaha kwa Israel
Waziri Kiongozi wa Scotland Humza Yousaf ameitaka Serikali ya Uingereza kusitisha uuzaji wa silaha kwa utawala wa Israel kutokana na utawala huo wa Kizayuni kuendeleza mauaji ya kimbari ya raia Wapalestina katika Ukanda Gaza.
Katika mahojiano na Middle East Eye - chombo huru cha habari cha Mashariki ya Kati - Waziri Kiongozi wa Scotland amesema hakuna "uhalali" wa kuendelea kuipatia Israel silaha. "Nadhani Serikali ya Uingereza inahitaji kuacha kuipa Israeli silaha," alisema.
Ameongeza kuwa: "Sasa wanahitaji kuacha kuwapa Israeli silaha. Siwezi kuwa wazi zaidi kuhusu hilo kutokana na baadhi ya matukio ya kikatili ambayo tumeyaona ambayo bila shaka ni ukiukaji wa sheria za kibinadamu.
Yousaf amebainisha kwamba jinai zimeshuhudiwa katika vita vya Gaza ikiwa ni pamoja na raia wasio na hatia wanaopeperusha bendera nyeupe kuuawa kwa kupigwa risasi, ulipuaji wa kambi za wakimbizi na ulipuaji wa shule.
Aidha amesema hakuna shaka kuwa utawala wa Israel umewaua makumi ya maelfu ya wanawake na watoto wasio na hatia.
Waziri Kiongozi wa Scotland amesema hakuna chochote kinachoweza kuhalalisha hatua ya Uingereza kuendelea kukabidhi silaha kwa jeshi na serikali ambayo imehusika katika ukiukwaji wa wazi wa sheria za kibinadamu."
Alipoulizwa atafanya nini ili kuhakikisha mitazamo yake inatekelezwa kivitendo, Yousaf amesema ataiandikia barua serikali ya Uingereza.
Yousaf ameongeza kuwa tishio la uvamizi wa nchi kavu huko Rafah limechangia uamuzi wake wa kutaka Uingereza ikomeshe mara moja uuzaji wa silaha kwa Israel.
Waziri Kiongozi wa Scotland amesema: "Ukweli sasa ni kwamba tuna tishio, tishio la kweli, kutoka kwa utawala wa Israel, la kufanya uvamizi wa nchi kavu huko Rafah, eneo ambalo lina mamilioni ya wanaume, wanawake na watoto wasio na hatia.
Amesema: Kuna tishio kwamba, sambamba na kuanza mwezi wa Ramadhani, mwezi mtukufu zaidi katika kalenda ya Waislamu, kutaanza uvamizi ambao utasababisha mauaji makubwa.
Amesema watu wasijifanye hawaelewi kuwa yanayojiri Gaza ni mauaji ya umati. Baada ya kipande cha video cha mahojiano hayo kusambazwa Middle East Eye, Yousaf alichapisha ujumbe kwenye X/Twitter kuthibitisha kwamba alikuwa amemwandikia barua Waziri Mkuu wa Uingereza Rishi Sunak. Katika ujumbe wake amesema "Serikali ya Uingereza lazima iache kutuma silaha kwa Israel."