Kiongozi Muadhamu: Iran haina wala haihitaji vikosi vya niaba
-
Imam Khamenei
Kiongozi wa Mapinduzi ya Kiislamu Ayatullah Sayyid Ali Khamenei amepuuzilia mbali madai kwamba Iran imefungiwa njia ya kufikia "vikosi vyake vya niaba" katika eneo la Magharibi mwa Asia, na kusisitiza kuwa Jamhuri ya Kiislamu haina wala haihitaji vikosi hivyo ili kufikia malengo yake
Ayatullah Sayyid Ali Khamenei, amesema hayo leo mbele ya hadhara ya wasomaji wa tungo za kuwasifu Ahlul-Bayt wa Mtume (SAW) kwa mnasaba wa maadhimisho ya kuzaliwa Bibi Fatima (AS), binti kipenzi wa Mtume Muhammad (SAW).
Kiongozi Muadhamu amesisitiza kuwa wapiganaji wa Kambi ya Muqawama nchini Yemen, na harakati kama vile Hizbullah ya Lebanon, na Hamas na Jihad Islami ya Palestina, yanapigana kwa sababu ya imani yao.
Imam Khamenei amesema kuwa: “Wao (maadui) mara kwa mara wanasema kwamba Jamhuri ya Kiislamu imepoteza washirika wake wa kieneo, hili ni kosa jingine! Jamhuri ya Kiislamu haina vikosi vya niaba."
Amesema wapiganaji wa muqawama, “wanasukumwa na imani zao; wanapigana kwa sababu ya imani yao, si kwa niaba yetu.”
Pia ameeleza kuwa iwapo Iran itaamua kuchukua hatua, haitahitaji nguvu ya wakala au niaba kufanya hivyo.
Kuhusiana na hali ya Syria, Kiongozi Muadhamu amesema katika mustakabali kutaibuka "mfumo imara na wenye heshima".
Ameongeza kuwa njama za Marekani za kutawala nchi zinahusisha kuanzisha udikteta au kuzua machafuko na ghasia, na mfano wa hivi karibuni ni Syria
Amesema: "Wamarekani, utawala wa Kizayuni wa Israel na washirika wao wanaamini kimakosa kuwa wameibuka washindi, jambo ambalo limewafanya watoe kauli za kipuuzi."
Kiongozi wa Mapinduzi ya Kiislamu alikuwa akiashiria matamshi ya afisa wa Marekani ambaye alionekana kuahidi uungaji mkono kwa yeyote anayechochea machafuko nchini Iran.
Ayatullah Khamenei amesema: "Taifa la Iran litamkanyaga chini ya miguu yake yenye nguvu mtu yeyote ambaye atachukua jukumu la mamluki wa Marekani katika suala hili."