Kamanda wa Jeshi: Iran inajiundia aghalabu ya silaha na zana za kivita
Kamanda Mkuu wa Jeshi la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesisitiza kuwa, Iran hivi sasa inajiundia aghalabu ya silaha na zana za kivita inazohitaji.
Meja Jenerali Seyed Abdolrahim Mousavi, Kamanda Mkuu wa Jeshi la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ameyasema hayo katika mahojiano na Shirika la Habari la IRIB na kuongeza kuwa hakuna wasiwasi wowote katika ulinzi wa Iran kwani aghalabu ya silaha na zana za kijeshi zimeundwa hapa nchini kwa ajili ya kukabiliana na adui.
Meja Jenerali Mousavi ameendelea kusema kuwa, kutokana na kujitolea muhanga Kikosi cha Ulinzi wa Anga katika zama za Kujihami Kutakatifu, tarehe 10 Shahrivar au Septemba Mosi ilitangazwa na Amiri Jeshi Mkuu kuwa Siku ya Kujihami Angani.
Kamanda Mkuu wa Jeshi la Iran ameongeza kuwa, Iran imepokea vitisho kutoka kwa maadui wakiongozwa dola katili la Marekani na pia utawala wa Kizayuni wa Israel na halikadhalika maadui wengine na kuongeza kuwa, vitisho hivyo vimepelekea Iran iimarishe uwezo wake wa kijeshi.
Amebainisha kuwa, kutokana na azma yake ya kuwa na kiwango cha juu cha zana za kujihami, Iran haijategemea uwezo wa kigeni.
Meja Jenerali Mousavi amesema kuimarika uwezo wa Majeshi ya Iran ukiwemo ule wa Kikosi cha Ulingi wa Anga, wataalamu wa masuala ya kijeshi sasa wanaamini kuwa, Iran ina kikosi bora zaidi cha ulinzi wa anga katika eneo la Magharibi mwa Asia.