WHO yaeleza wasiwasi wake kuhusu mgogoro wa afya nchini Yemen
Shirika la Afya Duniani (WHO) limeeleza wasiwasi wake mkubwa kuhusu uhaba mkubwa wa dawa, nishati na wahudumu wa masuala ya afya nchini Yemen.
Ripoti iliyotolewa jana na Shirika la Afya Dunia imesema kuwa, mashambulizi yanayoendelea kufanywa na Saudi Arabia nchini Yemen yameharibu kabisa hospitali na vituo 274 vya afya na kwamba kwa sasa asilimia 45 tu ya hospitali na vituo vya tiba ndiyo inayofanya kazi nchini humo.
WHO imekumbusha kuwa, hospitali na vituo vya afya nchini Yemen haviwezi kutoa huduma za matibabu kwa wagonjwa kutokana na uhaba wa dawa na chakula.
Ripoti za Umoja wa Mataifa zinasema kuwa, maelfu ya raia wasio na hatia wengi wao wakiwa wanawake na watoto wadogo wameuawa nchini Yemen katika mashambulizi ya Saudi Arabia na washirika wake.
Saudi Arabia ikiungwa mkono na Marekani na washirika wao wa Kiarabu na Kimagharibi walianzisha mashambulizi dhidi ya taifa la Yemen mwaka 2015 kwa shabaha ya kumrejesha madarakani kibaraka wao aliyetoroka nchi, Abdrabbuh Mansur Hadi.