Erdogan: Marekani ichague ima Fathullah Gulen au Uturuki
Katika kile kinachoonekana kuendelea kuingia doa uhusiano kati ya Ankara na Washington, Rais wa Uturuki ametoa machaguo mawili kwa Marekani.
Rais Recep Teyyip Erdogan amesema kuwa Ankara itasitisha ushirikiano wake wa kistratejia na Washington iwapo Marekani itaendelea kumpa hifadhi Fathullah Gulen, shakhsia wa kidini anayeipinga serikali ya Uturuki ambaye yuko uhamishoni nchini Marekani. Akizungumza katika Ikulu ya Rais mjini Ankara, Rais Erdogan amesema Marekani haina budi kuchagua ima kuendelea kuwa na uhusiano mzuri na Uturuki au iendelee kumpa hifadhi shakhsia huyo wa kidini ambaye Uturuki inamtuhumu kuwa gaidi mwenye misimamo ya kuchupa mipaka.
Rais Recep Teyyip Erdogan amesema serikali yake imeitumia Marekani mafaili 85 kuthibitisha kuwa Gulen alihusika na jaribio hilo la mapinduzi lililofeli mwezi uliopita. Hata hivyo, Gulen mwenye umri wa miaka 75 amekanusha kuhusika na jaribio hilo la mapinduzi.
Erdogan amekuwa akisisitiza kuwa, jaribio hilo la mapinduzi lilifanywa na nchi za Magharibi na kwamba tukio hilo lisingeweza kuongozwa na kuratibiwa kutoka ndani tu ya nchi. Watu wasiopungua 246 waliuawa huku wengine zaidi ya 2,100 wakijeruhiwa katika jaribio hilo la mapinduzi ya kijeshi la Julai 15.