Mkutano wa Usalama wa Mtandao Barani Afrika wafunguliwa Niamey, Niger
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i128744-mkutano_wa_usalama_wa_mtandao_barani_afrika_wafunguliwa_niamey_niger
Mkutano wa Afrika wa Usalama wa Mtandao ujulikanao kama “Kupeana Mkono kwa Ajili ya Mustakabali wa Kidijitali” umefunguliwa rasmi jijini Niamey, mji mkuu wa Niger, ukiwaleta pamoja wadau kutoka pembe mbalimbali za bara la Afrika.
(last modified 2025-07-25T07:26:05+00:00 )
Jul 25, 2025 07:26 UTC
  • Mkutano wa Usalama wa Mtandao Barani Afrika wafunguliwa Niamey, Niger

Mkutano wa Afrika wa Usalama wa Mtandao ujulikanao kama “Kupeana Mkono kwa Ajili ya Mustakabali wa Kidijitali” umefunguliwa rasmi jijini Niamey, mji mkuu wa Niger, ukiwaleta pamoja wadau kutoka pembe mbalimbali za bara la Afrika.

Mkutano huu, unaojulikana rasmi kama AfricaCERT–Handshake 25 Symposium, unalenga kuimarisha ushirikiano kati ya watafiti, taasisi, na watunga sera katika sekta ya usalama wa mitandao.

Waziri Mkuu wa Niger,  Ali Mahamane Lamine Zeine, alihudhuria ufunguzi wa mkutano huo siku ya Alhamisi, akiutaja kama jukwaa muhimu la kuhamasisha matumizi bora ya teknolojia ya kidijitali na kubadilishana uzoefu kati ya mataifa ya Afrika.

Mkutano huu una dhamira ya kuwezesha majadiliano ya kina kuhusu mbinu bora, uzoefu uliopatikana, na changamoto zinazokumba usalama wa mtandao na ulinzi wa taarifa, si tu barani Afrika bali pia duniani kote.

Aidha, tukio hili limeweka msingi wa kushirikiana kati ya timu za kukabiliana na matukio ya usalama mtandaoni (CSIRTs), maafisa wa usalama wa TEHAMA, na viongozi wa serikali kwa lengo la kujenga uimara wa pamoja dhidi ya mashambulizi ya mtandaoni.

Katika kipindi cha siku tatu za mkutano, washiriki wanahudhuria pia mafunzo maalum na warsha zinazolenga kuboresha ujuzi wa wataalamu wa usalama wa mtandao pamoja na viongozi wa maamuzi.

Vikao pia vinahusisha mijadala ya kutunga sera madhubuti za usalama wa mitandao zinazozingatia viwango vya kimataifa huku zikiendana na hali halisi na changamoto za kikanda.

Akizungumza na waandishi wa habari pembeni mwa mkutano huo, Mkurugenzi wa Shirika la Kitaifa la TEHAMA Niger, Bi Anne Rachel Marcel Inné, alisema: “Tunapaswa kupiga hatua katika zama za kidijitali, lakini kwa njia sahihi: kila kitu lazima kiwe salama. Ni muhimu kuwahusisha wananchi waelewe kuwa dunia ya kidijitali si tu kuwa kwenye WhatsApp, bali pia ni kuhusu miundombinu nyuma ya hayo yote , ambayo tunajenga kwa ajili ya Niger yenye mamlaka kamili ya kidijitali.”