Muungano wa wafanyakazi Nigeria watishia mgomo ikiwa serikali itapuuza matakwa yake
Muungano mmoja wa wafanyakazi nchini Nigeria umetishia kufanya mgomo wa nchi nzima ikiwa serikali ya Rais Muhammadu Buhari itaendelea kupuuza matakwa yake.
Joe Ajavero, Mkuu wa Muungano huo unaoitwa 'Kongresi ya Umoja wa Wafanyakazi' ametangaza kwamba, wanachama wa muungano huo watafanya mgomo huo kulalamikia hali mbaya na mishahara midogo wanayopewa wafanyakazi. Kwa mujibu wa Joe Ajavero, kuna uwezekano mgomo huo wa muungano wa wafanyakazi nchini humo ukaathiri kwa kiasi kikubwa sekta tofauti zikiwemo za mafuta na usafiri wa anga.
Kongresi ya Umoja wa Wafanyakazi ni kundi lililojitenga kutoka Umoja asili wa Wafanyakazi nchini Nigeria ambapo wanachama wake wako katika sekta tofauti kuanzia gesi, mawasiliano, usafirishaji, benki na umeme. Inafaa kuashiria kwamba, mbali na Nigeria kukabiliwa na matatizo ya kiusalama kutokana na mashambulizi ya kila mara ya wanachama wa kundi la kigaidi na ukufurishaji la Boko Haram, inakabiliwa pia na matatizo ya kiuchumi ambayo yaliongezeka baada ya kushuka bei ya mafuta katika soko la dunia.