Waasi wa Niger Delta watishia kuzishambulia taasisi za mafuta
Kundi la waasi kwa jina la "Walipizaji Kisasi wa Niger Delta" limetishia kuzishambulia taasisi za mafuta za nchi hiyo siku chache zijazo.
Waasi hao wa Niger Delta leo wameitahadharisha serikali ya Nigeria kuhusu hatua yake ya kupuuza matakwa ya vijana wa eneo huko kusini mwa nchi hiyo na kusisitiza kuwa watazidisha mashambulizi yao dhidi ya taasisi za mafuta na taasisi nyingine za kiuchumi za nchi hiyo.
Malalamiko ya jamii na uasi wa silaha umeongezeka katika eneo la niger Delta kusini mwa Nigeria kutokana na kuweko wimbi kubwa la vijana wasio na kazi na pia hatua ya serikali na viongozi wa nchi hiyo ya kupuuza matakwa ya tabaka hilo la vijana katika eneo tajiri kwa mafuta la kusini mwa nchi hiyo. Kundi hilo la waasi kwa jina la Walipizaji Kisasi Niger Delta limehusika na mashambulizi mengi dhidi ya taasisi za mafuta katika eneo hilo tajiri kwa mafuta huko kusini mwa Nigeria tangu mwaka 2016 hadi sasa. Mashambulizi hayo yamesababisha kupungua uzalishaji wa mafuta wa Nigeria.