UN yalaani mauaji ya askari wake 8 wa kulinda amani Kongo DR
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i49555-un_yalaani_mauaji_ya_askari_wake_8_wa_kulinda_amani_kongo_dr
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres amelaani mauaji ya askari 8 wa kikosi cha kulinda amani cha umoja huo katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.
(last modified 2026-02-21T22:51:18+00:00 )
Nov 16, 2018 11:19 UTC
  • UN yalaani mauaji ya askari wake 8 wa kulinda amani Kongo DR

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres amelaani mauaji ya askari 8 wa kikosi cha kulinda amani cha umoja huo katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

Kupitia msemaji wake, Stephane Dujarric, Katibu Mkuu wa UN sanjari na kutoa mkono wa pole kwa familia za wanajeshi hao wa Umoja wa Mataifa waliouawa na wanamgambo wa ADF, ametoa mwito wa kufikishwa mbele ya sheria wahusika wa jinai hiyo na kufanyika jitihada za kuyapokonya silaha magenge ya wapiganaji.

Amesema wanajeshi saba raia wa Malawi na mmoja wa Tanzania ndio waliouawa katika hujuma hiyo ya ADF huko Beni katika eneo la Kivu Kaskazini, huku 10 kijeruhiwa na mmoja akitoweka.

Amesema askari hao wa Kofia Buluu wa UN wameuawa wakiwa katika operesheni ya pamoja na vikosi vya serikali ya Kongo DR ya kulitokomeza kundi hilo la wapiganaji mashariki wa DRC. 

Katibu Mkuu wa UN, Antonio Guterres

Mwishoni mwa mwezi uliopita, wapiganaji hao wa Uganda walifanya tena mashambulio dhidi ya ngome za jeshi la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na kuua watu 13 mbali na kuwateka nyara watoto wasiopungua 12.

Aidha tarehe 22 Septemba pia raia 14 na wanajeshi 4 wa serikali ya Kongo DR  waliuawa katika shambulio lililodaiwa kufanywa na waasi wa Uganda wa ADF, mwezi mmoja baada ya genge hilo kufanya mashambulio mengine katika jimbo la Kivu Kaskazini mashariki mwa DRC na kuua watu sita.

Waasi wa Uganda wa ADF walianzisha harakati zao mashariki mwa Kongo tangu mwaka 1994 na katika miaka hiyo yote wameuwa mamia ya raia wa eneo hilo.