Feb 21, 2024 07:45 UTC
  • Amir-Abdollahian: Israel inahatarisha usalama wa Asia Magharibi

Hussein Amir-Abdollahian, Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa wa Iran amesema kuwa, utawala haramu wa Israel umehatarisha usalama wa eneo la Asia Magharibi.

Abdollahian amesema hayo katika mkutano na waandishi wa habari akiwa pamoja na Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Sri Lanka, Ali Sabri mjini Colombo hapo jana na kupongeza misimamo ya Sri Lanka ya kujiunga na azimio la Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa linalotaka kusitishwa mara moja mauaji ya kimbari na jinai za kivita za  utawala wa Kizayuni katika Ukanda wa Gaza na Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran pia aliunga mkono hatua ya serikali ya Afrika Kusini ya kuwasilisha shauri la mashtaka dhidi ya utawala wa Kizayuni  katika Mahakama ya Kimataifa ya Haki (ICJ) na kueleza kuwa, makubaliano yaliyofikiwa katika Umoja wa Afrika ya kuiunga mkono Palestina yana maslahi kwa Iran.

 

Akibainisha tukio la hivi karibuni la kuweka nanga meli mbili za Iran katika Pwani ya Sri Lanka, Amir Abdollahian amesema: Iran inaunga mkono usalama wa baharini na meli katika Ghuba ya Uajemi na Bahari ya Hindi na katika eneo kwa ujuma.

Kuhusu uhusiano mzuri na wa kirafiki uliopo kati ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na Sri Lanka na mashauriano yanayoendelea kati ya nchi hizo mbili kuhusu masuala ya pande mbili, kieneo na kimataifa, Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Iran ameeleza matumaini yake kuwa uhusiano kati ya nchi hizo mbili utapanuka zaidi katika nyanja zote, zikiwemo za kisiasa, kiuchumi, kibiashara na utalii.

Tags