Amir Abdollahian: Netanyahu amefika mwisho wa mstari
https://parstoday.ir/sw/news/iran-i109770-amir_abdollahian_netanyahu_amefika_mwisho_wa_mstari
Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema kuwa Benyamin Netayahu Waziri Mkuu wa utawala wa Kizayuni wa Israel amefikia mwisho wa barabara.
(last modified 2024-03-22T03:26:58+00:00 )
Mar 22, 2024 03:26 UTC
  • Amir Abdollahian: Netanyahu amefika mwisho wa mstari

Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema kuwa Benyamin Netayahu Waziri Mkuu wa utawala wa Kizayuni wa Israel amefikia mwisho wa barabara.

Hossein Amir Abdollahian jana usiku alizungumza kwa simu na Ismail Haniyeh Mkuu wa Ofisi ya Kisiasa ya Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina (Hamas) na kusema: Inaeleweka kwa ulimwengu kwamba Netanyahu amefika mwisho wa mstari na anafanya juhudi za mfamaji.

Benjamin Netanyahu 

Hossein Amir Abdollahian ameongeza kusema kuwa: Kama alivyosisitiza Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu, utawala wa Israel umenaswa katika kinamasi cha vita vya Gaza kutokana na misimamo ya wananchi na Muqawama wa Palestina.  

Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amemfahamisha Haniyeh kuhusu mashauriano ya karibuni na hatua za kidiplomasia za Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, ikiwa ni pamoja na kushiriki kikamilifu katika mikutano ya kimataifa kuhusu Palestina. 

Wakati huo huo, Amir abdollahian amelikosoa vikali Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa na kusisitiza kuwa, ipo haja kwa taasisi husika za kimataifa kuchukua hatua haraka iwezekanayo ili kusitisha mauaji ya kimbari ya raia wasio na hatia wakiwemo wanawake na watoto wa Gaza na Ukingo wa Magharibi mwa Mto Jordan. Amesema taasisi husika za kimataifa zinapaswa kuchukua hatua kuhakikisha kuwa misaada ya kibinadamu inatumwa haraka na bila ya vizuizi kwa wakazi wote wa Ukanda wa Gaza. 

Kwa upande wake, Ismail Haniyeh, Mkuu wa Ofisi ya Kisiasa ya Hamas, amewasilisha salamu zake njema kwa Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi na Rais wa Iran, na kutoa mkono wa kheri na fanaka kwa serikali na taifa la Iran kwa kuwadia  mwaka mpya wa Hijria Shamsia na mwezi Mtukufu wa Ramadhani. Vilevile amezungumzia matukio ya karibuni ya kisiasa na katika uwanja wa vita huko Gaza.