Abbas Araghchi: Marekani inafanya njama za kudhoofisha nchi za Kiislamu
Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Iran amesema kuwa, kinachofanywa na Marekani kwa kukiuka kwa kiasi kikubwa misingi na kanuni za sheria za kimataifa ni kwa niaba ya utawala wa Kizayuni na katika fremu ya mpango wao wa pamoja wa kuziangamiza na kuzidhoofisha nchi za Kiislamu na kulitawala eneo hili.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran Seyed Abbas Araghchi alilaani mashambulizi ya Marekani, Uingereza na utawala wa Kizayuni dhidi ya Yemen katika mazungumzo ya simu na Jamal Ahmed Ali Amer, Waziri wa Mashauri ya Kigeni na Wahajiri wa Yemen.
Huku akishukuru muqawama na uungaji mkono wa heshima wa wananchi wa Yemen kwa wananchi madhulumu wa Palestina, Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran ameongeza kuwa, utawala wa Kizayuni licha ya jinai na hujuma zake zote na kupata uungaji mkono usio na kikomo wa Marekani na baadhi ya nchi nyingine za Magharibi kinara wao akiwa Marekani, haujaweza kufikia malengo yake maovu.
Kwa upande wake, Jamal Ahmad Ali Amer Waziri wa Mashauri ya Kigeni na Wahajiri wa Yemen amesema kkuwa, njama za Marekani na Israel ni kuliweka eneo hili chini ya udhibiti wao, na nchi kubwa za Kiislamu na mataifa yanapaswa kutumia uwezo wao mkubwa kuwazuia wasifikie malengo yao.