Walowezi wa Kizayuni wauhujumu Msikiti wa Al Aqsa
https://parstoday.ir/sw/news/west_asia-i83282-walowezi_wa_kizayuni_wauhujumu_msikiti_wa_al_aqsa
Walowezi wa Kizayuni wameuhujumu Msikiti wa Al Aqsa katika mji wa Quds (Jerusalem) kwa mnasaba wa utawala haramu wa Israel kukalia kwa mabavu ardhi za Palestina.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
May 05, 2022 05:34 UTC
  • Walowezi wa Kizayuni wauhujumu Msikiti wa Al Aqsa

Walowezi wa Kizayuni wameuhujumu Msikiti wa Al Aqsa katika mji wa Quds (Jerusalem) kwa mnasaba wa utawala haramu wa Israel kukalia kwa mabavu ardhi za Palestina.

Kwa mujibu wa taarifa ya Iran Press, makundi ya walowezi wa Kizayuni yametoa wito kwa Wazayuni kuingia kwa nguvu katika Msikiti wa Al Aqsa Alhamisi ya leo kwa mnasaba wa kile wanachodai kuwa eti ni 'siku ya uhuru'.

Utawala wa Kizayuni umefungua lango la Al Aqsa lijulikanalo kama Bab al Magharibah na kuwaruhusu Wazayuni kuingia katika eneo hilo takatifu la Waislamu.

Kufuatia hatua hiyo ya kichochezi, Harakati ya Fatḥ, imetoa wito kwa Wapalestina wote wajitokeze kukabiliana na Wazayuni.

Gazeti la Rai al Youm limeandika kuwa Harakati ya Fath iko tayari kusimama kidete kukabiliana na uchokozi na uvamizi wa Wazayuni dhidi ya mji wa Quds, na maeneo mengine ya Palestina kwa kutumia njia zozote ziwezekanazo na zinazotambulika kwa mujibu wa sheria za kimataifa.

Fath imetoa wito kwa Wapalestina kuswali katika Msikiti wa Al Aqsa na kupeperusha bendera za Palestina katika maeneo mbali mbali ya msikiti huo sambamba na kukabiliana na hujuma za walowezi wa Kizayuni.

Eneo la Msikiti wa Al Aqsa mjini Quds

Harakati ya Fath inasisizia kuhusu muungano wa Wapalestina sambamba na kukabiliana na njama zote za Wazayuni za kuvuruga umoja huo. 

Jana Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina (Hamas) ilitahadharisha kuhusu vitendo vya kichochezi vya Wazayuni katika Msikiti wa Al-Aqsa na kusema vitendo hivyo ni sawa na kucheza na moto.

Hamas imetoa taarifa na kutangaza kuwa, hujuma yoyote dhidi ya Msikiti wa Al-Aqsa italielekeza eneo la Magharibi mwa Asia katika hali ambayo baraza la mawaziri la Israel ndilo litakalobeba dhima ya kuhusika nayo. 

Hamas imewataka Wapalestina shujaa kuhudhuria kwa wingi katika Msikiti wa al Aqsa na kuwa tayari kulinda utambulisho, dini na kibla chao cha kwanza cha Waislamu.

Msikiti wa Al-Aqsa ambao ni nembo kuu ya utambulisho wa Kiislamu na Palestina wa mji wa Quds (Jerusalem), daima umekuwa ukilengwa kwa vitendo vya uharibifu vya utawala haramu wa Israel na walowezi wa Kizayuni.