Marekani yajitoa tena katika UNESCO kwa sababu ya Palestina
https://parstoday.ir/sw/news/world-i128658
Marekani imeamua kujiondoa katika Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) kwa mara ya pili kwa sababu ya uamuzi uliochukuliwa na shirika hilo la UN wa kuikubali Palestina kuwa nchi mwanachama.
(last modified 2025-07-23T07:21:20+00:00 )
Jul 23, 2025 07:21 UTC
  • Marekani yajitoa tena katika UNESCO kwa sababu ya Palestina

Marekani imeamua kujiondoa katika Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) kwa mara ya pili kwa sababu ya uamuzi uliochukuliwa na shirika hilo la UN wa kuikubali Palestina kuwa nchi mwanachama.

Naibu Katibu wa Habari wa Ikulu ya White House Anna Kelly alitangaza uamuzi huo katika taarifa aliyotoa jana Jumanne na kueleza kwamba sababu ya kufanya hivyo ni kuunga mkono UNESCO mipango inayotekelezwa ambayo kuwa haiendani na maslahi ya Marekani.
 
"Rais Trump ameamua kuiondoa Marekani katika UNESCO - ambayo inaunga mkono sababu za upendeleo, zinazoleta migawanyiko ya kitamaduni na kijamii ambazo haziendani kabisa na sera za utimamu wa akili ambazo Wamarekani walipigia kura mnamo Novemba," ameeleza Kelly.

Naye msemaji wa wizara ya mambo ya nje ya Marekani Tammy Bruce amesisitiza kuwa kubaki katika UNESCO si kwa maslahi ya kitaifa ya Washington, akishutumu shirika hilo kuwa eti lina "ajenda ya kimataifa, ya kiitikadi ya maendeleo ya kimataifa inayokinzana na sera ya kigeni ya Marekani Kwanza".

Ameendelea kueleza kwamba kupokelewa Palestina kama nchi mwanachama na UNESCO kunatazamwa kuwa ni tatizo kubwa na ni kinyume na sera ya Marekani, na hivyo kuchangia kuongezeka utoaji kauli zilizo dhidi ya Israel ndani ya shirika hilo.

Mkurugenzi Mkuu wa UNESCO Audrey Azoulay amesema amesikitishwa na uamuzi wa Trump kujiondoa katika shirika hilo, lakini akaongeza kuwa hilo lilitarajiwa, na kwamba UNESCO ilishajitayarisha nalo.

Hatua hiyo ni pigo kwa UNESCO ambayo ilianzishwa baada ya Vita vya Pili vya Dunia kwa lengo la kuhimiza amani kupitia ushirikiano wa kimataifa katika elimu, sayansi na utamaduni.

Marekani ilijiondoa kwenye UNESCO wakati wa muhula wa kwanza wa Trump lakini ilijiunga tena katika kipindi cha rais wa zamani Joe Biden.../