Wahajiri 1,400 waokolewa Bahari ya Mediterranea wakielekea Ulaya
https://parstoday.ir/sw/news/world-i20020-wahajiri_1_400_waokolewa_bahari_ya_mediterranea_wakielekea_ulaya
Wahajiri 1,400 aghalabu kutoka kaskazini mwa Afrika, wameokolewa baada ya boti zao kuzama katika Bahari ya Mediterranea wakielekea barani Ulaya.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Nov 23, 2016 04:42 UTC
  • Wahajiri 1,400 waokolewa Bahari ya Mediterranea wakielekea Ulaya

Wahajiri 1,400 aghalabu kutoka kaskazini mwa Afrika, wameokolewa baada ya boti zao kuzama katika Bahari ya Mediterranea wakielekea barani Ulaya.

Gadi ya Pwani ya Italia iliyotekeleza operesheni hiyo ya jana Jumanne imesema wahamiaji hao haramu ambao safari yao ilianzia nchini Libya walikuwa  wakisafiri katika boti ndogo  za plastiki zipatazo 11 wakati waokoaji walipowaona wakizama na kwamba miili minane imepatika katika operesheni hiyo ya uokoaji.

Wapiga mbizi hao wa Italia wamesema watatu kati ya manusura wa ajali hiyo wapo katika hali mbaya na kwamba wanahitaji huduma za dharura za matibabu.

Wahajiri wa Kiafrika wakielekea Ulaya

Haya yanajiri siku chache baada ya wahajiri wengine wapatao 550, akthari yao wakitokea Afrika Magharibi, kuokolewa kutoka katika  Bahari ya Mediterranea wakielekea Italia.

Hii ni katika hali ambayo, Shirika la Kimataifa la Wahamiaji limetangaza kuwa, kiiwango cha maafa ya wahajiri baharini kimeongezeka mara sita mwezi huu wa Novemba ikilinganishwa na mwezi kama huu mwaka jana.

Shirika hili hivi karibuni lilisema kuwa, idadi ya wahajiri waliopoteza maisha yao katika Bahari ya Mediterranean imepindukia watu 4,636. Kwa mujibu wa takwimu rasmi za shirika hilo, tangu mwanzoni mwa mwaka huu 2016, karibu wahajiri laki tatu na 43 elfu na 589 wameingia barani Ulaya kwa njia ya baharini.