Idadi ya watu wasio na makazi wala nyumba yavunja rekodi Marekani
(last modified Mon, 26 Dec 2016 04:28:51 GMT )
Dec 26, 2016 04:28 UTC
  • Idadi ya watu wasio na makazi wala nyumba yavunja rekodi Marekani

Ripoti iliyotolewa na Muungano wa Taifa kwa Ajili ya Kukomesha Hali ya Kutokuwa na Makazi nchini Marekani (National Alliance to End Homelessness) inaonesha kuwa, idadi ya watu wasio na makazi nchini humo imeongezeka kwa kiasi ambacho hakijawahi kushuhudiwa.

Ripoti ya muungano huo iliyotolewa jana Jumapili imesema kuwa, kila usiku Wamarekani zaidi ya laki tano na 60 elfu hulala nje mitaani. Ripoti hiyo imeongeza kuwa, idadi ya Wamarekani wanaolala nje na wasio na makazi katika mji wa New York imefikia kiwango cha juu sana baada ya kile kilichoshuhudiwa katika kipindi cha mdororo mkubwa wa uchumi wa mwaka 1930 nchini Marekani.

Maelfu ya Wamarekani wanalala mitaani

Takwimu hizo pia zinaonesha kuwa, Wamarekani 17 kati ya kila elfu kumi hawana nyumba wala makazi na wanalazimika kulala mitaani.

Takwimu hizo zinasema kuwa, wastani wa watu wasio na nyumba wala makazi nchini Marekani ni zaidi ya watu laki tano na kwamba laki 1 na elfu 25 kati yao ni watoto wadogo.

Takwimu zinaonesha kuwa mji wa Los Angeles ndio wenye idadi kubwa zaidi ya watu wasio na makazi nchini Marekani na kwamba karibu watu wote hao wanaishi mitaani.      

Tags