Marekani yatoa vitisho kwa waungaji mkono wa Korea Kaskazini
-
Nimrata "Nikki" Haley, mwakilishi wa Marekani katika Umoja wa Mataifa
Mwakilishi wa Kudumu wa Marekani katika Umoja wa Mataifa ametoa vitisho vikali kwa nchi zinazoiunga mkono wa Korea Kaskazini.
Nimrata "Nikki" Haley amesema hayo leo mbele ya waandishi wa habari katika ofisi za Umoja wa Mataifa mjini New York na kuongeza kuwa, nchi zinazoiunga mkono kisiasa Korea Kaskazini na kupinga siasa za Marekani, zijiandae kuwekewa vikwazo na Washington.
Haley amekwepa kuzungumzia siasa za kupenda vita za Marekani katika maeneo tofauti duniani na badala yake amedai kuwa eti nchi hiyo inapigania amani hivyo yeyote anayeiunga mkono Korea Kaskazini ajiandae kuwekewa vikwazo.
Vile vile ameichochea Russia ichukue misimamo iliyo dhidi ya Korea Kaskazini na kusema kuwa, Moscow inapaswa kuwa na wasiwasi sana kutokana na majaribio ya makombora yanayofanywa na Korea Kaskazini kwani katika majaribio ya hivi karibuni, makombora ya Korea Kaskazini yalitua karibu tu na mpaka wa Russia.
Siku ya Jumapili, Korea Kaskazini ilifanyia majaribio makombora yake ya balestiki katika eneo la kaskazini magharibi mwa nchi hiyo.
Pyongyang inasema kuwa imefanya majaribio hayo ili kujikinga na chokochoko za kijeshi za Marekani na waitifaki wake. Imesisitiza kuwa, itaimarisha makombora yake pamoja na silaha zake za nyuklia kwa ajili ya kukabiliana na mashambulizi yanayoweza kufanywa na Marekani na waitifaki wake dhidi ya nchi hiyo.