Jumatatu, 15 Aprili, 2024
Leo ni Jumatatu tarehe 6 Shawwal 1445 Hijria sawa na tarehe 15 Aprili mwaka 2024.
Katika siku kama ya leo miaka 659 iliyopita, alifariki dunia Ibn Bardes, malenga na mpokezi wa Hadithi wa Kiislamu.
Ibn Bardes alizaliwa huko Baalbek moja kati ya miji ya Lebanon na kuelekea katika mji wa Damascus Syria baada ya kukamilisha masomo yake ya awali, ambapo alinufaika na elimu ya maulamaa maarufu wa zama hizo. Msomi huyo wa Kiislamu alisafiri katika nchi mbalimbali za Kiislamu na akaanza kufundisha baada ya kukamilisha masomo yake. Alikuwa mashuhuri baina ya watu kwa kushikamana na dini, kutakasa nafsi na maadili mema. Miongoni mwa vitabu vya Ibn Bardes ni al I'amu fii Wafayatil Aalam.

Siku kama ya leo miaka 572 iliyopita, alizaliwa mchoraji na msanii mashuhuri wa kutengeneza vinyago wa Italia Leonardo da Vinci.
Alionesha kipaji kikubwa cha kuchora akiwa bado mtoto mdogo na alikweya daraja za juu katika fani hiyo haraka mno. Mbali na uhodari wake katika kuchora na kutengeneza vinyago, Leonardo da Vinci pia alisomea fizikia na hisabati.
Miongoni mwa kazi zake mashuhuri ni michoro ya Kanisa Kuu la mji wa Milan, mchoro wa picha ya "Tabasamu la Jugund," picha ya Mona Lisa na ya Karamu ya Mwisho ya Issa Masih (as). Leonardo da Vinci alifariki dunia mwaka 1519 akiwa na umri wa miaka 67. *
Siku kama ya leo miaka 112 iliyopita meli kubwa ya abiria ya Titanic ambayo ilitambuliwa kuwa nembo ya mafanikio makubwa ya viwanda vya meli vya wakati huo iligonga mwamba wa theluji na kugharibi katika Bahari ya Atlantic, katika safari yake ya kwanza kutoka bandari ya Southampon nchini Uingereza ikielekea New York, Marekani.
Zama hizo Titanic ilitambuliwa kuwa meli kubwa zaidi na ya kifahari kuliko zote duniani. Watengenezaji wa meli hiyo walikuwa akisema kuwa haiyumkini kughariki na kuzama. Wasafiri 705 tu kati ya abiria wake wote 2207 ndio waliookoka katika ajali hiyo.
Ajali hiyo inatambuliwa kuwa mbaya zaidi ya baharini na iliyosababisha idadi kubwa ya vifo duniani.
Siku kama ya leo miaka 36 iliyopita, yaani sawa na tarehe 15 Aprili 1988, shirika la ujasusi la utawala bandia wa Israel MOSSAD lilimuua shahidi Khalil al Wazir maarufu kwa jina la Abu Jihad mwasisi na shakhsia nambari mbili wa Harakati ya Ukombozi ya Palestina PLO huko Tunis, Tunisia.
Abu Jihad aliongozana na wenzake nchini Misri, na huko wakaamua kuanzisha harakati ya mapambano dhidi ya Wazayuni, na kuipatia jina la Harakati ya Ukombozi ya Palestina PLO.
Tarehe 15 Aprili miaka 30 iliyopita, ulitiwa saini mkataba wa kuanzisha Shirika la Biashara Duniani (WTO) nchini Morocco.
Utangulizi wa kuasisiwa shirika hilo ulifanywa na Marekani na Uingereza wakati wa Vita vya Pili vya Dunia na kwa msingi huo, mwaka 1947 nchi 23 zilizoendelea zilitia saini makubaliano ya kuanzisha GATT. Makubaliano hayo yalisisitiza juu ya kufanyika mazungumzo ya kupunguza ushuru wa forodha, vipingamizi vya biashara na kuondoa vizuizi vya biashara huru.
Baadaye jumuiya ya GATT ilibadilishwa jina na kuwa WTO na hati yake ilianza kutekelezwa Januari mwaka 1995. Hata hivyo Marekani na nchi nyingine za Magharibi zimeliteka shirika hilo la kibiashara duniani na kulitumia kwa faida na maslahi yao wenyewe.
