Jul 01, 2018 21:59 UTC
  • Jumatatu 2 Julai 2018

Leo ni Jumatatu 18 Shawwal 1439 sawa na 2 Julai 2018

Siku kama ya leo miaka 185 iliyopita Mirza Hussein Nuri, alimu na faqihi mashuhuri wa Kiislamu alizaliwa katika mji wa Nur kaskazini mwa Iran. Baada ya kukamilisha masomo yake ya awali, Mirza Hussein Nuri alielekeza juhudi na jitihada zake katika masuala ya kujifunza na kukusanya hadithi. Msomi huyo wa Kiislamu alitokea kuwa mmoja wa wasomi wakubwa wa masuala ya hadithi na baadaye akaanza kuandika vitabu vya thamani katika uwanja huo.

irza Hussein Nuri

Miaka 93 iliyopita katika siku kama hii ya leo alizaliwa Patrice Lumumba mhandisi wa uhuru wa Kongo. Lumumba alitoa mchango mkubwa katika juhudi za kukombolewa Kongo wakati wa harakati za ukombozi wa nchi za Kiafrika. Lumumba aliteuliwa kuwa Waziri Mkuu na Waziri wa Ulinzi baada ya kuundwa Jamhuri ya Kongo mwaka 1960. Patrice Lumumba aliuawa mwaka 1961 na vibaraka wa Marekani na Ubelgiji baada ya kuvumilia mateso na unyama mkubwa. Lumumba aliandika vitabu kadhaa wakati wa uhai wake na mashuhuri zaidi ni kile alichokita "Kongo, Nchi Yangu."

Patrice Lumumba

Tarehe Pili Julai miaka 57 iliyopita aliaga dunia mwandishi mtajika wa Kimarekani kwa jina la Ernest Hemingway. Alizaliwa mwaka 1899 na kwa muda fulani alikuwa mwandishi huko Uingereza na Ufaransa.Hemingway alianzisha mbinu ya kuandika riwaya na tungo fupi fupi na alikuwa akitumia lugha nyepesi na inayoeleweka. Mwaka 1954 mwandishi Ernest Hemingway alitunukukiwa tuzo ya Nobel katika medani ya fasihi.Miongoni mwa vitabu maarufu vya Hemingway ni "The Old Man and The Sea", "A Farewell to Arms" na For Whom The Bell Tolls".

Ernest Hemingway

Na tarehe 11 Tir miaka 36 iliyopita Ayatullah Muhamad Saduqi alimu mkubwa, mwanamapambano na Imamu wa Ijumaa wa mji wa Yazd huko katikati mwa Iran, aliuawa shahidi na vibaraka wa kundi la kigaidi la Munafiqiin na kuwa shahidi wa nne aliyeuawa katika mihrabu ya swala katika historia ya Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran. Ayatullah Muhammad Saduqi alikamilisha masomo yake ya kidini katika Hauza ya mji mtakatifu wa Qum, Iran na kustafidi na bahari kubwa ya elimu kutoka kwa walimu mashuhuri wa kituo hicho cha kielimu kama vile Ayatullah Burujerdi na Ayatullah Khansari.

Ayatullah Muhamad Saduqi