Hadithi ya Uongofu (29)
Ni matumaini yangu kuwa, hamjambo wapenzi wasikilizaji na karibuni katika sehemu nyingine ya kipindi cha Hadithi ya Uongofu. Kipindi hiki kama tulivyotangulia kusema hapo kabla, hujadili maudhui mbalimbali na kunukuu baadhi ya hadithi zinazohusiana na maudhui hizo.
Kwa hakika dini tukufu ya Kiislamu imelipa umuhimu mkubwa na wa hali ya
juu, suala la kujipamba na sifa nzuri za kimaadili na kiakhlaqi kama
kusaidia watu, kuwa mkarimu, kufanya juhudi kwa ajili ya kutatua
matatizo ya wengine na kukidhi hawaiji na shida za watu. Kipindi chetu
cha juma hili ambacho ni sehemu ya 29 ya mfululizo huu kitazungumzia
sifa na tabia hii njema na ya kupendeza. Ni matumaini yangu kuwa,
mtakuwa nami hadi mwisho wa kipindi hiki kusikiliza yale
niliyokuandalieni kwa leo.
Kila Mwislamu anapenda kufahamu
ibada bora kabisa ili kwa kuzitekeleza ibada hizo apate njia ya karibu
kabisa ya kupata radhi za Mwenyezi Mungu. Tab'an, Mwenyezi Mungu ni
mpole na Mwenye huruma na kabla hata ya waja wake, ni mwenye kupenda
amali zao njema na kujikurubisha kwao kwake.
Imepokewa katika riwaya
na hadithi kutoka kwa Bwana Mtume (s.a.w) na Ahlul-Bayt wake watoharifu
(a.s) kwamba, kukidhi shida na haja za waumini ni miongoni mwa amali
njema na zenye thamani ya hali ya juu. Amali hii imetajwa katika baadhi
ya riwaya kwamba, ni zaidi ya kuwakomboa watumwa elfu moja katika njia
ya Mwenyezi Mungu na ni bora kuliko kuwatayarisha na kuwapeleka katika
medani ya vita wapiganaji elfu moja.
Imam Ja'afar Swadiq (a.s)
amesema: Mtu ambaye atachukua hatua kwa ajili ya kukidhi haja ya muumini
ili kutaka ujira wa Mwenyezi Mungu na akafanikiwa kutekeleza hilo, basi
Mwenyezi Mungu Mtukufu atamuandikia ujira na thawabu za sawa na kuhiji
na kufanya Umra, thawabu za kufunga Saumu miezi miwili na kukaa itikafu
katika miezi mitukufu katika Masjid al-Haram huko Makka. Na mtu ambaye
amenuia kufanya hivyo lakini hakufanikiwa kutekeleza nia yake hiyo ya
kukidhi na kutekeleza haja na shida ya nduguye muumini, Mwenyezi Mungu
humuandikia thawabu za Hija moja maqbuul. Hivyo basi kimbilieni kufanya
wema na hisani."
Pamoja na hayo nukta ya kuzingatiwa hapa katika hili
ni kwamba, kufanya amali hiyo ya wema na hisani licha ya thamani yote
iliyonayo, katu jambo hilo haliwezi kuchukua nafasi ya jukumu na wadhifa
mwingine wa kidini. Na hakuna mtu anayeweza kuacha kutekeleza mambo ya
wajibu katika dini kama Swala na mengineyo kwa kusingizio cha kumhudumia
kiumbe. Kwa hakika katika dini tukufu ya Kiislamu kila amali ina
thamani kwa nafasi yake na analopaswa kuzingatia mwanadamu ni kutekeleza
yale ambayo yana kipaumbele kulingana na mafundisho ya Uislamu.
Imam
Ja'afar Swadiq (a.s) amenukuliwa akisema kuwa: Amali bora kabisa ni
maarifa na kumtambua Muumba wa ulimwengu. Kisha Swala, Zaka, Saumu,
Hija; na maarifa juu yetu sisi Ahlul Bayt (a.s) ndio amali iliyo bora
zaidi. Kisha kuwafanyia wema na hisani ndugu katika dini ni katika amali
bora kabisa."
Kwa hakika mtu ambaye anatatua shida na kukidhi
mahitaji na hawaiji za watu, mbali na kupata radhi za Mwenyezi Mungu
huwafurahisha pia waja wa Allah na wakati huo huo hupata utukufu na
ubora duniani na akhera. Mtume (s.a.w) amesema: Mtu bora miongoni mwa
watu ni yule ambaye ana faida na manufaa kwa watu wengine."
Nabii Issa Masih (a.s) naye amesema akiwa mtoto kwamba:
"Na
amenijaalia ni mwenye kubarikiwa popote pale niwapo". Katika kufasiri
aya hiyo ya 31 ya Surat Maryam, Imam Ja'afar Swadiq amesema: Kubarikiwa
hapa ina maana ya mwenye kuwanufaisha watu wengine. Ndio maana huku
kuwanufaisha watu wengine hupelekea mtu kuwa mwenye kubarikiwa.
Katika
Uislamu kutatua shida ya Mwislamu imetambuliwa kuwa amali na kitendo
ambacho kina msingi wa kumfurahisha Mwenyezi Mungu na vile vile Mtume
wake (s.a.w). Imekuja katika hadithi mashuhuri kwamba, Mwenyezi Mungu
ana nafasi katika nyoyo zenye imani. Aidha katika upande mwingine
imepokea katika Hadith al-Qudsi kutoka kwa Mwenyezi Mungu ya kwamba
amesema: Watu ni familia yangu, hivyo wapendwa zaidi kwangu miongoni
mwao ni wenye huruma zaidi kwa familia yangu na ambao wanafanya hima na
idili zaidi kwa ajili ya kutatua shida na hawaiji za watu."
Kwa
hakika hadithi hizi mbili zinabainisha nukta muhimu mno nayo ni kwamba,
kila mtu ambaye analeta furaha na nishati katika nyoyo za watu, Mwenyezi
Mungu hufurahi na kumridhia na anakuwa ametoa zawadi ya amali nzuri
kabisa mbele ya Mwenyezi Mungu.
Mtume (s.a.w) amesema: Kila mtu
ambaye atamfurahisha muumini, amenifurahisha mimi, na kila mwenye
kunifurahisha mimi amemfurahisha Mwenyezi Mungu."
Kwa hakika
kumfurahisha Mwenyezi Mungu ambako kuna maana ya kumridhisha Mwenyezi
Mungu na kupata radhi zake, hupelekea mtu kupata rehma maalumu za
Mwenyezi Mungu. Tab'an, wanadamu wote wananufaika na ujazi na neema za
Mwenyezi Mungu, lakini kuna baadhi ya watu kutokana na ustahiki wao
wanaouonesha kutokana na kutenda amali njema, hujumuishwa katika rehma
maalumu za Mwenyezi Mungu. Mtume (s.a.w) amesema:
Mtu ambaye
atamuonyesha na kumrimu ndugu yake Mwislamu kwa neno zuri na la heshima
na akamtatulia shida zake, basi huwa chini ya kivuli cha rehma za
Mwenyezi Mungu madhali angali katika hali ya kufanya amali hiyo."
Miongoni
mwa athari za kuwasaidia watu wengine na kushughulikia shida na
matatizo yao ni mja kusamehewa dhambi zake. Hapana shaka kuwa, katika
kipindi chote cha maisha hapa duniani sote wakati fulani huteleza na
kutenda dhambi. Kufanya toba na kujutia dhambi ni njia bora kabisa ya
mja kusamehewa na kufutiwa dhambi zake. Pamoja na hayo, kutenda wema na
hisani, nayo ni amali yenye taathira katika kusamehewa dhambi za mtu.
Mwenyezi Mungu anasema katika aya ya 14 ya Surat Hud:
"Hakika mema huondoa maovu."
Je kwa kuzingatia aya hiyo na hadithi zilizotangulia, kuna wema na jema gani bora zaidi ya kusaidia waja wa Mwenyezi Mungu?
Imam Ali bin Abi Twalib (a.s) anasema:
Kafara ya dhambi kubwa ni kuitikia mayowe ya wenye shida na matatizona kutatua shida za waliokwama (katika mambo yao).
Imam
Ja'afar Swadiq (a.s) amesema kuwa: Shindaneni katika kufanya amali
njema na kuweni ni waja wa hilo. Hakika peponi kuna mlango ambao jina
lake ni "Maarufu" ambao haingii kupitia mlango huo isipokuwa watu
waliofanya wema na hisani.
Wapenzi wasikilizaji, muda wa kipindi
chetu cha leo umefikia tamati hivyo sina budi kukomea hapa, nikitaraji
kuwa mtakuwa nami wiki ijayo katika sehemu nyingine ya kipindi chetu
hiki cha Hadithi ya Uongofu.
Wassalaamu Alaykum Warahmatullahi Wabarakaatuh.