Alkhamisi, Juni 15, 2023
Leo ni Alkhamisi tarehe 26 Mfunguo Pili Dhulqaada 1444 Hijria inayosadifiana na tarehe 15 Juni mwaka 2023 Milaadia.
Miaka 722 iliyopita katika siku kama hii ya leo, alizaliwa faqihi, mfasiri, mtaalamu wa teolojia na mwanafasihi wa Kiislamu, Mas'ud bin Omar Taftazani huko Quchan, Kaskazini mwa Iran. Kwa kipindi kirefu cha umri wake, Taftazani alifanya safari katika miji ya Khorasan na Asia ya Kati kwa lengo la kutafuta elimu. Allamah Taftazani alianza kuandika vitabu akiwa bado kijana kutokana na uhodari na umahiri wake, na baadhi ya vitabu vya msomi huyo mkubwa wa Kiislamu vingali vinafundishwa hadi hii leo. Miongoni mwa vitabu hivyo ni al Mutwawwal, al Irshad na Mukhtasarul Maani.

Tarehe 15 Juni miaka 315 iliyopita katika siku kama ya leo harakati ya wapigania uhuru wa Scotland ilikandamizwa vikali na Uingereza. Uingereza daima imekuwa ikifanya jitihada za kuiunganisha Scotland na ardhi ya kaskazini mwa nchi hiyo. Hata hivyo harakati za mapambano za Wascotland zilipinga vikali suala hilo. Hata hivyo mwaka 1707 mabunge ya nchi hizo mbili yaliunganishwa. Suala hilo liliwakasirisha sana Wascotland walioanzisha harakati nyingine ya mapambano mbayo ilikandamizwa vikali katika siku kama ya leo hapo mwaka 1708.
Siku kama ya leo miaka 175 iliyopita sawa na tarehe 15 Juni 1848, Otto von Bismarck Kansela wa Ujerumani aliuchagua mji wa kihistoria na maarufu wa Berlin, kuwa mji mkuu wa nchi hiyo. Kuteuliwa mji wa Berlin kuwa mji mkuu wa Ujerumani, kulitokana na utekelezaji wa mpango wa kuziunganisha Ujerumani mbili, uliobuniwa na Kansela Bismarck. Baada ya Vita vya Pili vya Dunia, Ujerumani iligawanyika katika sehemu mbili za Mashariki na Magharibi. Mwezi Septemba 1990 baada ya kuvunjwa ukuta wa Berlin, kuliandaliwa mazingira ya kuunganishwa pande hizo mbili, na hatimaye Berlin kurejea tena na kuwa mji mkuu wa Ujerumani.
Siku kama ya leo miaka 28 iliyopita, mwafaka na tarehe 15 Juni 2000, idadi kubwa ya askari wa kikosi maalumu cha jeshi la Uingereza iliondoka kwenye ardhi ya Sierra Leone, magharibi mwa Afrika. Amri ya kuondoka vikosi hivyo vya Uingereza ilitangazwa na John Prescott, Naibu Waziri Mkuu wa Uingereza. Wanajeshi wengine 300 wa nchi hiyo waliendelea kubaki nchini Sierra Leone kwa wiki kadhaa kwa shabaha ya kutoa mafunzo kwa jeshi la nchi hiyo.