Apr 29, 2024 07:19 UTC
  • Viongozi wa Afrika wanakutana Nairobi Kenya kujadili miradi ya maendeleo

Marais na viongozi wa serikali wa nchi mbalimbali kutoka mataifa tofauti ya bara la Afrika, wanakutana jijini Nairobi kwenye mkutano wa Kimataifa wa Maendeleo kwa ushirikiano na Benki ya Dunia (IDA).

Mbali na viongozi wa nchi mbalimbali, mkutano huo unahudhuriwa na viongozi wa mashirika ya kiraia, vijana na wadau wengine wa maendeleo, kujadiliana kuhusu miradi ya maendeleo inayopaswa kutekelezwa barani Afrika kwa kupata msaada na ufadhili wa wadau wa maendeleo.

Ripotii zinaeleza kuwa, mpango huo wa maendeleo ya kimataifa, unaoshirikiana na Benki ya Dunia, una miradi kwenye nchi 75 duniani.

Baada ya kuundwa mwaka 1960, lengo la muungano huo ulikuwa ni kusaidia mataifa masikini kupambana na umasikini kwa kuwezesha utoaji wa mikopo kwa riba ya chini kwa ajili ya maendeleo ya kiuchumi, kuweza usawa na kuboresha maisha ya watu.

Mbali na Benki ya Dunia, mataifa zaidi ya 30, yakiwemo China, Chile, India, Korea Kusini na Uturuki, ni miongoni mwa nchi wafadhili wa mradi huo.

Katika mwaka wa fedha uliokamilika Juni 2023, IDA ilitoa Dola Bilioni 34.2 kwa ajili ya msaada, huku mataifa ya Afrika yakipokea asilimia 75 ya fedha hizo kwa ajili ya maendeleo.