Somalia yakanusha madai ya Marekani ya kutwaa chakula cha WFP
Somalia jana Alhamisi ilikanusha madai ya Marekani kwamba maafisa wa eneo hilo wametwaa bidhaa za chakula kutoka katika ghala la shirika la Mpango wa Chakula Duniani (WFP), huku Washington ikisimamisha misaada kwa Mogadishu kusubiri uchunguzi.
Wizara ya Mambo ya Nje ya Somalia imesema kuwa bidhaa hizo za chakula zilizotajwa kwenye ripoti ni zilikuwa chini ya usimamizi wa WFP.
Taarifa ya Wizara ya Mambo ya Nje ya Somalia imeeleza kuwa ghala la WFP liko katika eneo la Bandari ya Mogadishu, ambapo upanuzi unaoendelea na ujenzi mpya haujaathiri uhifadhi, usimamizi au usambazaji wa misaada ya kibinadamu.
Wizara hiyo imesema: Serikali inachunguza madai hayo ya Marekani kupitia kamati ya kiufundi kwa kushirikiana na washirika wa masuala ya kibinadamu kufuatia wasiwasi uliojitokeza kuhusu shughuli za upanuzi wa bandari hiyo.
Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani Jumatano iliyopiita ilisema Washington imesitisha misaada yote kwa serikali ya Shirikisho ya Somalia baada ya kudai kuwa maafisa wa eneo hilo wameharibu ghala la Mpango wa Chakula Duniani (WFP) na kutwaa tani 76 za chakula kilichokusudiwa kwa ajili ya raia wa Kisomali walio hatarini.