Rais wa Nigeria kureja nyumbani baada ya matibabu London
Rais Muhammadu Buhari wa Nigeria anatarajiwa kurejea nyumbani baada ya matibabu ya wiki kadhaa London, Uingereza.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa Jumanne na Ikulu ya Rais wa Nigeria, mke wa Buhari, Bi. Aisha Buhari amewashukuru Wanigeria kwa kumuombea mume wake na kusema, "atarejea nyumbani hivi karibuni kwani anapona haraka."
Buhari aliondoka Abuja Mei 7 kwa duru ya pili ya matibabu mjini London na kabla ya kuondoka alimuachia mamlaka kamili makamu wake, Yemi Osinbajo ili kuepusha pengo la madaraka katika nchi hiyo yenye uchumi mkubwa zaidi Afrika.
Itakumbukwa kuwa, mwezi Machi mwaka huu, Buhari alirejea nchini Nigeria akitokea mjini London ambako alikuwa likizo kwa muda wa siku 51 kwa ajili ya matibabu.
Hii ni katika hali ambayo, serikali na familia ya Buhari haijaweka wazi kuhusu ugonjwa unaomsumbua rais huyo wa Nigeria mwenye umri wa miaka 74.