SUPKEM Kenya yataka kuweko mfumo mmoja wa masomo kwa shule za Kiislamu
Baraza Kuu la Waislamu nchini Kenya SUPKEM limetoa wito wa kuandaliwa mfumo mmoja wa masomo kwa ajili ya shule za Kiislamu katika nchi hiyo ya Afrika Mashariki.
Katika mkutano wake uliofanyika katika msikiti wa Jamia jijini Nairobi, Baraza Kuu la Waislamu nchini Kenya limesisitiza kwamba, kuna haja ya kuandaliwa mfumo mmoja wa masomo kwa ajili ya shule za Kiislamu nchini humo tofauti na sasa ambapo kila shule imekuwa na mfumo wake wa masomo.
Baraza hilo la SUPKEM limezitaka taasisi zote za masomo na utafiti za Kiislamu nchini Kenya ziandae mfumo mmoja jumuishi wa masomo katika viwango vyote katika shule za Kiislamu na kukabidhi kwa Wizara ya Elimu kama mpango wa masomo kwa ajili ya shule za Kiislamu.
Pendekezo hilo la Baraza Kuu la Waislamu nchini Kenya SUPKEM linatolewa katika hali ambayo, serikali ya nchi hiyo mwaka 2012 ilizitambua rasmi shule, na madrasa za elimu ya dini zinazoendeshwa na kufundishwa kulingana na matashi ya wamiliki.
Baraza la Supkem sambamba na kuashiria kuwa, licha ya kuwa, vituo hivyo vya elimu havina ratiba maalumu iliyotayarishwa lakini limesisitiza kuwa, vituo vya kielimu vinapaswa kufanya kazi vikiwa na umoja na mshikamano.
Waislamu nchini Kenya wanaunda takribani asilimia 30 ya jamii ya nchi hiyo ya Afrika Mashariki.