Umoja wa Mataifa waonyesha matumaini ya kufikiwa makubaliano ya amani Sudan Kusini
Mjumbe wa Umoja wa Mataifa katika masuala ya Sudan Kusini ameeleza matarajio yake juu ya kufikiwa makubaliano ya amani ya kuhitimisha machafuko nchini humo katika mazungumzo yanayoendelea hivi sasa mjini Addis Abab, Ethiopia.
David Shearer amesema, licha ya kwamba serikali na wapinzani wa nchi hiyo wanaendelea na hujuma za hapa na pale, lakini kuna matumaini ya kuendelea vyema mazungumzo hayo ya amani nchini Ethiopia. Amesisitiza kuwa, katika mazungumzo ya Ijumaa ya leo ambayo yatahusu masuala ya usalama, katiba na serikali kuna uwezekano mkubwa kukapigwa hatua nzuri kwa ajili ya taifa hilo changa zaidi barani Afrika.
Mazungumzo kati ya serikali ya Sudan Kusini na wapinzani yalianza tarehe tano ya mwezi huu mjini Addis Ababa, Ethiopia.
Sudan Kusini ilijitenga na Sudan mwaka 2011 baada ya miongo kadhaa ya mapigano makali ya kutaka kujitenga na Khartoum. Hata hivyo tangu mwaka 2013 nchi hiyo ilitumbukia katika hali ya mchafukoge baada ya Rais Salva Kiir Mayardit kumtuhumu makamu wake wa zamani, Riek Machar kwamba alikula njama za kutaka kumpindua. Katika vurugu hizo maelfu ya watu wameuawa na mamilioni ya wengine kuwa wakimbizi ndani na nje ya nchi hiyo.