Maandamano yafanyika nchini Algeria kwa wiki ya pili mfululizo
Maelfu ya raia wa Algeria wamefanya maandamano kwa wiki ya pili mfululizo kulalamikia siasa za serikali ya nchi hiyo.
Maelfu ya Waalgeria walimiminika katika mitaa ya mji mkuu Algiers jana Jumamosi kupinga siasa za serikali ya nchi hiyo, licha ya serikali kupiga marufuku maandamano hayo na kutuma mamia ya askari kwa ajili ya kuyazuia, kwa kisingizio cha kuzuia maambukizi ya corona.
Waandamanaji wanataka viongozi wa hivi sasa waondoke madarakani na kuruhusu mabadiliko yafanyike katika muundo wa demokrasia ya nchi hiyo. Waandamanaji pia wanalalamikia mswada wa sheria unaoazimia kuwapokonya uraia Waalgeria wanaoishi nje ya nchi hiyo.
Algeria inaendelea kushuhudia misukosuko na mivutano ya kisiasa tokea wakati Abdul Aziz Bouteflika, rais wa zamani wa nchi hiyo alipoondolewa madarakani kutokana na mshinikizo ya wananchi na wanajeshi.
Waalgeria wanaamini kwamba uchaguzi wa rais uliofanyika tarehe 12 Disemba 2019 na kumuweka madarakani Rais Abdelmadjid Tebboune haukuwa na natija nyingine ghairi ya kuendeleza utawala wa zamani wa Abdul Aziz Bouteflika, ambapo viongozi wa hivi sasa wanaendeleza siasa zile zilezile za utawala huo wa zamani.