Oct 11, 2022 12:12 UTC
  • Al-Azhar yalaani kuchomwa moto Qurani na walowezi wa Kizayuni

Chuo Kikuu cha Kiislamu cha al Azhar cha nchini Misri kimelaani kile ilichokitaja kuwa ugaidi za Kizayuni, baada ya Walowezi wa Kiyahudi kuchoma moto Qurani Tukufu katika eneo la Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan, huko Palestina inayokaliwa kwa mabavu.

Taarifa iliyotolewa leo Jumanne na al-Azhar imeeleza kuwa, kitendo hicho cha kuvunjiwa heshima Qurani Tukufu kimefanyika katika anga ya kimya kisichokubalika cha jamii ya kimataifa.

Taasisi hiyo ya Kiislamu nchini Misri imesema katika tamko lake hilo kuwa, hatua hiyo ya Walowezi wa Kizayuni inaenda kinyume na sheria na kanuni za kimataifa, huku ikionya kuhusu matokeo mabaya ya uafriti huo.

Taarifa hiyo imebainisha kuwa: Al-Azhar Sharif inalaani kwa nguvu zote na kukosoa kitendo kiovu cha magaidi wa Kizayuni, katika mji wa al-Khalil (Hebron) huko Palestina, ambao walichana na kuchoma moto nakala za Qurani Tukufu, katika kitendo kilichoonesha ugaidi, ufuska na chuki za Kizayuni.

Kadhalika Chuo cha al-Azhar kimekosoa kimya kinachoonyeshwa na walimwengu mbele ya ugaidi wa kinyama wa Wazayuni dhidi ya Wapalestina wakazi wa Quds Tukufu na dhidi ya msikiti mtukufu wa Al-Aqsa na kusisitiza kuwa, kimya hicho kinatia aibu.

Chuo Kikuu cha Kiislamu cha al Azhar cha Misri kimetoa mwito wa kudumishiwa umoja na mshikamano miongoni mwa Waislamu na Waarabu, mkabala wa wanaoyavunjia heshima matukufu ya Kiislamu.

 

Tags