Jun 30, 2024 10:04 UTC
  • Walinzi wa Haram; waokozi wa Iran na eneo la Asia Magharibi

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema kuwa, Walinzi wa Haram ni tukio la kushangaza, muhimu na mojawapo ya madhihirisho ya mtazamo wa kiulimwengu wa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran.

Ayatullah Ali Khamenei alisema hayo Jumamosi ya jana (29 Juni 2024) katika kikao na wajumbe wa Kongamano la Kimataifa la Mashahidi wa Muqawama na Walinzi wa Haram na kubainisha kwamba, Walinzi wa Haram ni waokozi wa Iran na eneo la Asia Magharibi.

Kiongozi Muadhamu amesema kuwa, kuwepo vijana wa mataifa mbalimbali katika sura ya Walinzi wa Haram kulionyesha kuwa, Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran yana uwezo wa kuibua upya hamasa ya kipindi cha mwanzoni mwa mapinduzi hayo baada ya kupita zaidi ya miongo minne.

Ayatullah Khamenei amekutaja kushiriki wapiganaji wa harakati ya Walinzi wa Haram katika nchi ambazo adui alikuwa amepanga njama hatari sana dhidi yao kuwa ni mojawapo ya madhihirisho ya mtazamo wa kiulimwengu wa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran. Aidha amesema, katika mipango yake, adui alikuwa na lengo la kuangamiza utawala wa Kiislamu nchini Iran kwa kulikalia kwa mabavu eneo la Magharibi mwa Asia na wakati huo huo kuiwekea Iran mashinikizo ya kiuchumi, kisiasa, kiitikadi na kimadhehebu; lakini kundi la vijana wenye imani, chini ya uongozi wa Jamhuri ya Kiislamu, limezima na kubatilisha mpango huu wenye gharama kubwa wa kibeberu. Ayatullah Khamenei amesisitiza kuwa, kwa mtazamo huu inapasa kusema kuwa, hatua na harakati ya Walinzi wa Haram imeiokoa Iran na eneo la Asia Magharibi kwa ujumla.

 

Kiongozi Muadhamu akizungumza na wajumbe wa Kongamano la Kimataifa la Mashahidi wa Muqawama na Walinzi wa Haram

Katika matamshi ya Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu imesisitizwa hadhi na taathira za Walinzi wa Haram ambao katika miaka ya hivi karibuni wamekuwa na nafasi athirifu katika kukabiliana na makundi ya kigaidi likiwemo la Daesh licha ya njama mtawalia za Marekani na utawala wa Kizayuni. Baada ya mgogoro wa Syria, Marekani na utawala wa Kizayuni ziliingilia kati na kuzusha ukosefu wa usalama na ukosefu wa uthabiti katika eneo na kuyaunga mkono makundi ya kigaidi yaliyokuwa yakipigana vita vya niaba.  Lakini bila shaka, vikosi vilivyokuwa mstari wa mbele  na vyenye taathira na vilivyojitokeza kukabiliana na njama za Wazayuni na Magharibi katika eneo walikuwa Walinzi wa Haram.

Mgogoro wa Syria uliibuka mwaka 2011 kwa mashambulizi makubwa ya makundi ya kigaidi yanayoungwa mkono na Marekani na waitifaki wake kwa ajili ya kubadilisha milingano ya eneo kwa maslahi ya utawala wa Kizayuni.  Kwa ombi rasmi la serikali ya Syria, Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ilitoa msaada wa ushauri kwa nchi hiyo ya Kiarabu katika kukabiliana na magaidi.  Jeshi la Syria hatimaye liliweza kuwashinda magaidi wa kitakfiri wa Daesh kwa msaada wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na makundi ya muqawama.

Walinzi wa Haram walikuwa na mchango mkubwa  katika matukio ya eneo hili, na huo ukawa mwisho wa makundi ya kigaidi likiwemo na Daesh yaliyokuwa yakiungwa  mkono na Magharibi, huko Iraq na Syria. Hapana shaka kuwa, mafanikio hayo yalitokana na mchango na uwepo endelevu na mzuri Walinzi wa Haram huku Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ikiwa ndio kitovu chake na hivyo ikawezekana kulinda miji ambayo ilishambuliwa na magaidi na hata kudhibitiwa.

 

Makundi ya kigaidi na kitakfiri yakipata himaya na uungaji mkono mkubwa wa kifedha na silaha kutoka kwa Wamarekani na Wamagharibi, yaliweza kudhibiti sehemu za ardhi za Iraq na Syria na kwa kipindi kifupi yakasababisha maafa makubwa ya kibinadamu. Kwa mwongozo na uratibu wa Luteni Jenerali Haj Qassim Suleimani, Walinzi wa Haram waliweza kutoa vipigo visivyofidika dhidi ya makundi ya kigaidi na kuvisaidia vikosi vya kijeshi na vya wananchi nchini Syria na Iraq kukabiliana vyema na magaidi wa Daesh.

Katika hali ambayo nchi nyingi za eneo hili pia zilikuwa na wasiwasi kwamba zingekabiliwa na mzozo wa kiusalama kutokana na hatua za kundi la Daesh na waungaji mkono wao wa nchi za magharibi, vikosi vya Walinzi wa Haram kutoka Iran vilivyotumwa huko Syria na Iraq viliweza kudhamini usalama wa eneo na kusambaratisha kikamilifu njama za waungaji mkono wakuu wa makundi ya kigaidi.