Iran na China ni ngome isiyoweza kupenywa na vikwazo vya Marekani
Wizara ya Fedha ya Marekani imezidisha mashinikizo dhidi ya Tehran kwa kukiwekea vikwazo kiwanda cha kusafisha mafuta cha China kwa madai ya kununua mafuta ya Iran. Hata hivyo, takwimu zinaonyesha kuwa si tu vikwazo hivyo havijazuia mauzo ya mafuta ya Iran, bali pia vimezidisha ushirikiano wa kiuchumi na kijiografia kati ya Iran na China.
Shirika la Habari la Fars limeandika makala maalumu kuhusu suala hilo na kusema; Vikwazo vya Marekani dhidi ya kiwanda cha kusafisha mafuta cha Shandong Shengxin, ambacho kwa mujibu wa Idara ya Hazina ya Marekani, kilinunua mafuta yenye thamani ya zaidi ya dola milioni 800 kutoka kwa makampuni yenye uhusiano na Iran kati ya miaka ya 2020 na 2023, ni sehemu ya mbinu zinazotumiwa kufelisha vikwazo vya Washington.
Takwimu za satelaiti na ripoti za Umoja wa Mataifa zinaonyesha kuwa mauzo ya mafuta ya Iran yalifikia mapipa milioni 1.82 kwa siku mwezi Machi 2025. Ripoti ya TankerTrackers inasema kuwa asilimia 45 ya meli za mafuta za Iran zimekuwa zikikwepa vikwazo vya Marekani kwa kutumia mbinu tofauti.
Makala hiyo ya shirika la habari la FARS imeongeza kuwa: "Waraka wa siri kutoka benki kuu ya China unaonesha kuwa asilimia 32 ya manunuzi ya mafuta ya Iran yaliyopelekwa China yalifanywa kwa kutumia sarafu zisizo za dola. Makala hiyo imemnukuu Zhang Lian, mwanauchumi katika Chuo Kikuu cha Peking akisema: "Badala ya kuitenga Iran, vikwazo vya Marekani vimeigeuza Tehran kuwa ngome ya kuunda mifumo mbadala ya mabadilishano ya kifedha."
Makala hiyo pia imesema: "Hatua ya Marekani ya kujitoa katika mapatano ya JCPOA mwaka 2018 na kuyawekea vikwazo mashirika ya Ulaya yanayofanya kazi nchini Iran, kama vile Total, ilizua mpasuko kati ya Washington na washirika wake."
Pia limeandika: Vikwazo vya hivi sasa vya Marekani mbali na kuongeza mivutano baina yake na China, haviwezi kuidhoofisha Iran bali vinaonekana kuimarisha ushirikiano wa kambi nyingine kubwa katika mfumo wa kitaasisi kama vile Jumuiya ya Ushirikiano ya Shanghai na kundi la BRICS.