Sheikh Qassim: Imamu Khamenei alirejesha Umma kwenye Uislamu halisi
https://parstoday.ir/sw/news/iran-i138390-sheikh_qassim_imamu_khamenei_alirejesha_umma_kwenye_uislamu_halisi
Mwanazuoni mkuu wa Bahrain, Ayatullah Sheikh Isa Qassim amemsifu Kiongozi wa Mapinduzi ya Kiislamu aliyeuawa shahidi, Ayatullah Imam Ali Khamenei, kama "mtu aliyerudisha Umma kwenye Uislamu halisi."
(last modified 2026-05-16T02:53:12+00:00 )
May 16, 2026 02:52 UTC
  • Sheikh Qassim: Imamu Khamenei alirejesha Umma kwenye Uislamu halisi

Mwanazuoni mkuu wa Bahrain, Ayatullah Sheikh Isa Qassim amemsifu Kiongozi wa Mapinduzi ya Kiislamu aliyeuawa shahidi, Ayatullah Imam Ali Khamenei, kama "mtu aliyerudisha Umma kwenye Uislamu halisi."

Ayatullah Qassim alitoa matamshi hayo katika ujumbe uliorushwa kwenye televisheni kwa mnasaba wa tukio lililofanyika Ijumaa mjini Tehran ili kuzindua kitabu cha lugha ya Kiarabu cha "Hikayatu Sayyid" kuhusu kiongozi huyo aliyeuawa shahidi.

Ayatullah Sayyid Ali Khamenei aliuawa katika shambulio la kigaidi la Marekani na Israel dhidi ya Iran mnamo Februari 28. Wanafamilia kadhaa pia waliuawa shahidi katika shambulio hilo.

"Imam Khamenei alikuwa mtu hodari, mwenye uwezo na bidii katika kurudisha Umma kwenye Uislamu kwa dhati na kwa ikhlasi, na alifanikiwa kulinda umoja wa Umma wa Kiislamu katika njia yake sahihi, kwa mujibu wa mafundisho ya Uislamu," amesema mwanazuoni huyo wa Bahrain.

Katika sehemu nyingine ya ujumbe wake, Ayatullah Isa Qassim ameashiria kusambaratika ndoto na malengo mabaya ya madhalimu na madola ya kibeberu sambamba na ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamu nchini Iran, na kupoteza maslahi yao baada ya ushindi wa mapinduzi hayo.

Akizungumzia hofu iliyosababishwa na Mapinduzi ya Kiislamu katika safu za madola ya kibeberu kuhusu kuanzishwa serikali ya Kiislamu, amesema, "Hakuna hofu inayoweza kulinganishwa nayo, kwa sababu mfumo huu ni mfumo wa Kiislamu unaotumika kama mfano hai usio na kifani wa serikali ya haki, ya busara, yenye uwezo na salama inayoinua maisha ya roho na mwili; serikali inayofufua udugu wa binadamu na kufichua udhaifu, ufisadi na dhulma ya mifumo mingine ya kidhalimu duniani."

Amesema kwamba vita vya sasa vinajiri kati ya kambi ya ujinga na ujahilia ya imani, akisisitiza kwamba "hatamu ya uongozi wa kambi ya ujahilia iko mikononi mwa Marekani dhalimu, Uzayuni uliopotea, na Uyahudi ambao umeasi dini ya kweli ya Nabii Musa (amani Mungu iwe juu yake)."

"Kinara wa uongozi wa Marekani ni 'Firauni Trump,' na kiongozi wa Uzayuni ni 'Firauni Netanyahu.' Hawa wawili kwa sasa ni miongoni mwa waovu wabaya zaidi, wenye uadui zaidi kwa maadili na matukufu, ambao mikono yao imelowa damu zaidi za wanadamu, na wenye ukaidi zaidi mbele ya Mungu na makatazo Yake," amesema Sheikh Isa Qassim.