China iko tayari kusaidia kuimarisha usitishaji vita Syria
Mjumbe Maalumu wa China katika masuala ya Syria amekaribisha na kuunga mkono ubunifu wa Iran, Russia na Uturuki kwa ajili ya kusaidia kupunguza machafuko huko Syria na kueleza kuwa nchi yake iko tayari kutoa misaada inayohitajika ili kuimarisha usitishaji vita nchini humo.
Akizungumza jana Jumapili na Muhammad Irani Mkurugenzi katika Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran anayehusika na masuala ya Mashariki ya Kati na Kaskazini mwa Afrika, Xie Xiaoyan ameongeza kuwa mgogoro wa Syria unaweza kutatuliwa kwa njia za kisiasa na kufanyika mazungumzo kati ya Wasyria wenyewe kwa wenyewe.
Xie Xiaoyan amesema China inaunga mkono uhuru, mamlaka ya kujitawala ardhi nzima ya Syria na kusisitiza juu ya msimamo wa wazi wa nchi yake katika kupambana na makundi yenye misimamo mikali duniani. Xiaoyan amelaani pia uingiliaji wa nchi ajinabi katika masuala ya nchi nyingine duniani.
Katika mazungumzo hayo, naye Muhammad Irani amesisitiza kuwa Iran na China zina misimamo ya pamoja kuhusu matukio ya Syria na kusisitiza kuwa kuna udharura wa kuendelezwa mashauriano kati ya nchi mbili hizo ili kuhitimisha mgogoro wa Syria na kuwasaidia raia wa nchi hiyo katika mchakato wa kuijenga upya nchi yao.