Naibu balozi wa Iran UN: Ukosefu wa usalama unaongeza umasikini
https://parstoday.ir/sw/news/iran-i39795-naibu_balozi_wa_iran_un_ukosefu_wa_usalama_unaongeza_umasikini
Naibu balozi na mwakilishi wa kudumu wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran katika Umoja wa Mataifa amesema kuwa, ukosefu wa usalama na amani unachangia kuongezeka umasikini duniani.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Feb 02, 2018 00:36 UTC
  • Naibu balozi wa Iran UN: Ukosefu wa usalama unaongeza umasikini

Naibu balozi na mwakilishi wa kudumu wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran katika Umoja wa Mataifa amesema kuwa, ukosefu wa usalama na amani unachangia kuongezeka umasikini duniani.

Ishaq al-Habib, amesema hayo katika kikao cha 56 cha Kamisheni ya Ustawi wa Jamii ya Umoja wa Mataifa na kuongeza kuwa, licha ya kuchukuliwa hatua chanya kimataifa kwa ajili ya kupambana na umasikini, lakini bado kuna watu wengi katika maeneo mbalimbali duniani wanaoishi katika umasikini mkubwa.

Naibu balozi na mwakilishi wa kudumu wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran katika Umoja wa Mataifa ameashiria mizozo, migogoro, mapigano ya silaha na ukosefu wa amani katika maeneo mbalimbali ulimwenguni likiwemo eneo la Mashariki ya Kati  na kusisitiza kwamba, mizozo hiyo imekuwa na taathira kubwa katika kushadidisha umasikini hususan kwa wanawake na watoto.

Ishaq al-Habib, Naibu balozi na mwakilishi wa kudumu wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran katika Umoja wa Mataifa

Ishaq al-Habib, amesisitiza juu ya umuhimu wa kupewa kipaumbele suala la kupambana na umasikini na kueleza kwamba, suala hilo halipasi kufanywa wenzo wa mashinikizo ya kisiasa.

Amesema Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imeandaa mipango mbalimbali ya kupambana na umasikini katika fremu ya mpango wa sita wa miaka mitano ya ustawi wa kitaifa na kwamba, imepasisha na kuandaa mipango na sheria katika uwanja huo.

Kikao cha 56 cha kila mwaka cha Kamisheni ya Ustawi wa Jamii ya Umoja wa Mataifa kilianza tarehe 29 mwezi uliopita wa Januari na kinatarajiwa kuendelea hadi tarehe 7 mwezi huu.