Iran: Hatukaribishi vita lakini tuko tayari kujihami kwa nguvu zote
https://parstoday.ir/sw/news/iran-i54280-iran_hatukaribishi_vita_lakini_tuko_tayari_kujihami_kwa_nguvu_zote
Kamanda wa Kikosi cha Anga za Mbali cha Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu (SEPAH) amesema kuwa, majeshi na wananchi wa Iran hawataki vita lakini daima wako imara kuihami na kuilinda nchi yao.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Jun 22, 2019 07:40 UTC
  • Iran: Hatukaribishi vita lakini tuko tayari kujihami kwa nguvu zote

Kamanda wa Kikosi cha Anga za Mbali cha Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu (SEPAH) amesema kuwa, majeshi na wananchi wa Iran hawataki vita lakini daima wako imara kuihami na kuilinda nchi yao.

Brigedia Jenerali Amir Ali Hajizadeh amesema hayo leo Jumamosi katika mahojiano na shirika la habari la IRNA, na huku akiashiria kutunguliwa ndege ya kijasusi ya Marekani katika fukwe za kusini mwa Iran amesema, kitendo cha Marekani cha kufanya ujasusi ndani ya Iran ni kinyume cha sheria za kimataifa na kwamba hatua ya Iran ya kuitungua ndege hiyo ya kijasusi ya Marekani ilikuwa ni sehemu ya utekelezaji wa majukumu ya kisheria ya vikosi vya ulinzi vya Jamhuri ya Kiislamu.

Kamanda huyo wa Kikosi cha Anga za Mbali cha Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu ameongeza kuwa, majibu ya majeshi ya Iran kwa wavamizi wa anga ya nchi hii ni makali sana na iwapo uvamizi kama huo utatokea tena, Iran iko imara kutoa majibu mengine makali.

Mdege mkubwa wa kijasusi wa Marekani wa Global Hawk uliopopolewa na kusambaratishwa vipande vipande na kombora la Iran

 

Brigedia Jenerali Hajizadeh amesema pia kuwa katika kipindi cha miaka 40 iliyopita, Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imekuwa ikikabiliwa na hujuma za kila namna za maadui na kusisitiza kuwa: Usalama wa taifa na kulinda kila shibri ya ardhi ya nchi ni vipaumbele vikuu vya vikosi vya ulinzi vya Iran na kwamba leo hii Jamhuri ya Kiislamu inajitosheleza kwa vifaa vya ulinzi ikiwemo mifumo ya kujilinda kwa makombora.

Kabla ya hapo pia, Brigedia Jenerali Hajizadeh alitoa maelezo kamili kuhusu harakati za drone hiyo ya kijasusi ya Marekani ambayo ilianza safari yake ya kijasusi saa sita na dakika 14 Alhamisi  usiku ikitokea uwanja mmoja wa ndege za kivita wa Umoja wa Falme za Kiarabu kabla ya kutunguliwa saa 10 na dakika 5 alfajiri karibu na Kouh-e-Mobarak katika eneo la Jask mkoani Hormozgan kusini mwa Iran.