Rouhani: Uchaguzi wa rais Iran unaangaziwa kimataifa
Rais Hassan Rouhani wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema macho ya dunia yameelekezwa kwenye uchaguzi ujao wa rais nchini Iran.
Rais Hassan Rouhani aliyasema hayo Jumatano jana katika kikao chake cha kila wiki cha baraza la mawaziri na kuongeza kuwa kuwa: "Uchaguzi wa rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran unazingatiwa na watu wote katika upeo wa kimataifa." Ameongeza kuwa, masanduku ya kupigia kura ni fakhari ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kwani mfumo wa Jamhuri nchini Iran umejengeka katika msingi wa masanduku ya kupigia kura.
Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran pia amelaani vikali jinai za kinyama za utawala wa Kizayuni wa Israel dhidi ya watu wasio na hatia wa Palestina ambapo ametoa wito kwa nchi za Kiislamu zifanye kila ziwezalo kwa ajili ya kuokoa maisha ya watu wa Palestina wanaokabiliwa na hujuma za kila siku za utawala wa Kizayuni wa Israel.
Rouhani pia amekosoa utendaji wa Umoja wa Mataifa na Jumuiya ya Nchi za Kiarabu kuhusu kadhia ya Palestina na kusema: "Ni jukumu la nchi zote za Kiislamu kuwasaidia watu wa Palestina na hakuna shaka kuwa hilo likifanyika, Wapalestina watapata ushindi.
Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran pia ameashiria mazungumzo ya Tume ya Pamoja ya Mapatano ya Nyuklia ya JCPOA ambayo yanafanyika Vienna, na kusema: "Naliahidi Taifa la Iran kuwa mwisho wa mazungumzo ya Vienna ni ushindi kwa taifa la Iran."