Rais Raisi: Usalama na uwezo wa Iran unategemea kusimama imara wananchi
Rais Ebrahim Raisi amefanya mazungumzo kwa njia ya simu na familia ya Shahidi mlinzi wa usalama wa nchi na kueleza kwamba usalama na uwezo wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran unategemea kusimama imara wananchi na juhudi kubwa za maelfu ya Mashahidi, na akasisitizia umuhimu wa watu wote kuilinda na kuienzi rasilimali hiyo ya taifa.
Katika mazungumzo hayo, Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ametoa salamu za rambirambi kwa familia ya Shahidi Amir Ahmadi na kuuelezea utamaduni wa kujitolea mhanga na kufa shahidi kuwa ni miongoni mwa mambo muhimu yanayojenga nguvu za taifa la Iran na kuongeza kuwa: kile ambacho hadi sasa kimeifanya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ibaki na fahari na ushindi katika uga wa makabiliano yanayoendelea na kila aina ya vitisho, njama na vitendo vya uadui, ni rasilimali yake ya kijamii, kalima ya umoja na utamaduni wa kujitolea mhanga na kuwa tayari kufa kishahidi.