Iran: Diplomasia haikukomesha uwepo wa magaidi Iraq, tumelazimika kuushughulikia kijeshi
Ofisi ya uwakilishi wa kudumu wa Iran katika Umoja wa Mataifa imemwandikia barua Rais wa Baraza la Usalama la umoja huo kubainisha hoja na sababu ya kuchukua hatua za kijeshi dhidi ya makundi ya kigaidi yaliyoko nchini Iraq na kusisitiza kuwa diplomasia haikuweza kukomesha kuwepo kwa magaidi kaskazini ya nchi hiyo na ndio maana Iran imelazimika kutumia nguvu za kijeshi.
Katika barua yake hiyo, ofisi ya uwakilishi wa kudumu wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran katika Umoja wa Mataifa imebainisha pia kuwa: kwa kutilia maanani vitisho vya kigaidi vinavyoendelea kuwepo, Wizara ya Mambo ya Nje ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran iliwasilisha malalamiko makali tena mara kadhaa kwa kutuma waraka rasmi wa kidiplomasia kwa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iraq kuhusiana na kuendelea kuwepo magenge ya kigaidi, kambi zao za mafunzo, harakati yanazoendesha kwa uhuru na vitendo vyao vya uharibifu yanayofanya kutokea ndani ya ardhi ya Iraq.
Barua ya ofisi ya uwakilishi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran UN imeendelea kueleza kwamba: licha ya malalamiko na maonyo ya mara kwa mara ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, kwa masikitiko, mamlaka za eneo la kaskazini mwa Iraq hazikuchukua hatua madhubuti na za maana dhidi ya magaidi kulingana na taratibu za kimataifa.
Katika hali kama hiyo na kwa kutilia maanani mashambulizi ya kigaidi yanayoendelea kufanywa, Jamhuri ya Kiislamu ya Iran haikuwa na chaguo jengine isipokuwa kutumia haki yake ya kujilinda kwa mujibu wa sheria za kimataifa ili kuwahami wananchi wake, usalama wa taifa, mamlaka ya kujitawala na umoja wa ardhi yake yote.
Ofisi ya uwakilishi wa kudumu wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran katika Umoja wa Mataifa imetamatisha barua yake hiyo kwa kumtaka Rais wa Baraza la Usalama aiweke barua hiyo kwenye orodha ya nyaraka za baraza hilo.../