Marekani yaiwekea vikwazo vipya Iran, vyajumuisha Mwendesha Mashtaka Mkuu
https://parstoday.ir/sw/news/iran-i91986-marekani_yaiwekea_vikwazo_vipya_iran_vyajumuisha_mwendesha_mashtaka_mkuu
Wizara ya Fedha ya Marekani imeiwekea Iran vikwazo vipya kwa kisingizio cha ukiukaji wa haki za binadamu, katika kuendeleza uingiliaji wake wa masuala ya ndani ya Iran na kutekeleza sera ya mashinikizo ya juu zaidi dhidi ya Tehran.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Dec 22, 2022 04:09 UTC
  • Marekani yaiwekea vikwazo vipya Iran, vyajumuisha Mwendesha Mashtaka Mkuu

Wizara ya Fedha ya Marekani imeiwekea Iran vikwazo vipya kwa kisingizio cha ukiukaji wa haki za binadamu, katika kuendeleza uingiliaji wake wa masuala ya ndani ya Iran na kutekeleza sera ya mashinikizo ya juu zaidi dhidi ya Tehran.

Marekani inahesabiwa kuwa mwekaji mkubwa zaidi wa vikwazo duniani ikiwa na rekodi ndefu zaidi ya kuziwekea nchi zingine aina mbalimbali za vikwazo kwa ajili ya kufanikisha malengo na maslahi yake.
Kwa mujibu wa shirika la habari la IRNA; Wizara ya Fedha ya Marekani ilitangaza jana kuwa imeyaweka majina ya maafisa watano wa kijeshi wa Iran na kampuni yenye uhusiano na Jeshi la Polisi la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kwenye orodha yake ya vikwazo.
Jina la Hujjatul Islam Mohammad Jaafar Montazeri, Mwendesha Mashtaka Mkuu wa Iran, nalo pia limejumuishwa kwenye orodha hiyo mpya ya vikwazo vilivyotangazwa na wizara ya fedha ya Marekani.
Wizara hiyo ya Marekani imedai kuwa sababu ya kuwekwa vikwazo hivyo ni kukandamizwa na kuwekwa kizuizini wapinzani nchini Iran.
Mwendesha Mashtaka Mkuu Hujjatul-Islam Mohammad Jaafar Montazeri

Tangu yalipoanza machafuko nchini Iran, serikali ya Joe Biden haijaacha kuchukua kila hatua huku ikieleza kinagaubaga kwamba badala ya kujikita kwenye mazungumzo na muelekeo wa kidiplomasia ambao imekuwa ikiupigia upatu kila mara, itafuatilia zaidi machafuko yanayojiri Iran.

Washington imeamua pia kuendeleza sera za mashinikizo ya juu kabisa za utawala wa Donald Trump; na kwa ushirikiano wa waitifaki wake wa Magharibi, hadi sasa imeshaiwekea Iran vikwazo kadhaa kwa kisingizio cha haki za binadamu ili kuunga mkono machafuko yaliyojiri nchini.../