Kiongozi Muadhamu aonya kuhusu njama za maadui wa Iran
https://parstoday.ir/sw/news/iran-i9238-kiongozi_muadhamu_aonya_kuhusu_njama_za_maadui_wa_iran
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ametahadharisha juu ya njama za maadui wanaoazimia kukwamisha maendeleo ya Iran.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Jun 15, 2016 04:05 UTC
  • Kiongozi Muadhamu aonya kuhusu njama za maadui wa Iran

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ametahadharisha juu ya njama za maadui wanaoazimia kukwamisha maendeleo ya Iran.

Ayatullah Ali Khamenei amesema, hii leo ajenda kuu ya adui ni kukwamisha au kusimamisha kabisa uwezo wa Iran ya Kiislamu au kwa uchache kuzuia maendeleo yake. Akiongea katika mkutano na wakuu wa mihimili mitatu ya serikali hapa Tehran jana Jumanne, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema kuna haja kwa taifa hili kuimarisha uwezo wake katika nyuga mbali mbali. Amesema: "Nimekuwa nikikariri mara kwa mara kwamba lazima nchi hii ipige hatua kiuwezo sambamba na kutambua na kuzipa nguvu sekta zilizopo; na kwamba hapo ndipo maofisa wa serikali wanaweza kutaraji taifa hili liwe katika hali ya utulivu."

Kuhusu makubaliano ya nyuklia ya Vienna, Ayatullah Ali Khamenei ameashiria kuhusu vitisho vinavyotolewa na wagombea wa urais wa Marekani kwamba watafutilia mbali utekelezwaji wa makubaliano hayo na kusisitiza kuwa, Jamhuri ya Kiislamu itatoa jibu kali kwa hatua yoyote kama hiyo. Kiongozi Muadhamu amesema kuwa: "Sisi hatuwezi kukiuka Mpango Kamili wa Pamoja wa Utekelezaji (JCPOA), lakini endapo upande wa pili utakiuka kama wanavyodai wanaowania kiti cha rais nchini humo, iwapo watayachana makubaliano hayo, sisi tutayatia moto."

Ayatullah Khaemenei amekumbusha kuwa, uadui wa Marekani dhidi ya taifa hili ndiyo sababu kuu ya kupatikana Mapinduzi ya Kiislamu, jambo ambalo sio la mjadala.