Kesi ya shambulio la kemikali la Sardasht katika mahakama ya ICC
Majeruhi wa shambulio la kemikali katika mji wa Sardasht, kaskazini magharibi mwa Iran, amesisitiza kuwa kesi ya mashambulizi ya silaha za kemikali dhidi ya mji huo inafutiliwa katika katika Mahakama ya Kimataifa ya Jinai (ICC).
Wanajeshi wa utawala wa wakati huo wa Iraq wa Baath ambao walikuwa wakipigana na vikosi vya jeshi la Iran, mwaka 1987 walifanya shambulio la kinyama dhidi ya raia wasio na ulinzi wa mji wa Sardasht katika mkoa wa Azerbaijan Magharibi nchini Iran kwa kutumia silaha za kemikali za maangamizi ya umati zilizopigwa marufuku bila ya kuzingatia sheria za kimataifa.
Katika shambulio hilo la kemikali, jeshi la anga la utawala wa Saddam Hussein lilishambulia maeneo manne yenye wakazi wengi katika mji wa Sardasht kwa mabomu saba ya haradali, na kuuwa shahidi watu 130. Aidha watu zaidi ya elfu nane waliathiriwa na mashambulio hayo ya silaha za kemikali.
Shabnam Sheikhi, mmoja wa majeruhi wa hujuma ya Sardasht, ametoa ufafanuzi kuhusu shambulio hilo la kemikali na kusema vikwazo vimekuwa vikikwamisha pakubwa upatikanaji wa dawa kwa manusura walioathiriwa na mabomu ya kemikali. Amesema, Sardasht inapaswa kuwa nembo ya hujuma ya kinyama ya silaha za kemikali.
Majeruhi huyo wa shambulio la kemikali katika mji wa Sardasht ameeleza kuwa ameshiriki mikutano kadhaa ya Shirika la Kuzuia Silaha za Kemikali, na kwamba, alihudhuria mikutano hiyo kama waraka na ushahidi hai wa mashambulizi dhidi ya mji wa Sardasht.