Al-Burhan atembelea miji ya kimkakati ya Sudan iliyokombolewa kutoka kwa RSF
-
Al-Burhan atembelea miji ya kimkakati ya Sudan iliyokombolewa
Mwenyekiti wa Baraza la Mpito la Sudan Jenerali Abdel Fattah al-Burhan ametembelea miji ya Umm Sayala na Jabrat al-Sheikh katika jimbo la Kordofan Kaskazini siku moja baada ya jeshi kuchukua udhibiti wa maeneo mawili kutoka kwa wapiganaji wa RSF.
Taarifa iliyotolewa na baraza hilo imesema al-Burhan, ambaye pia ni mkuu wa majeshi, alikagua vikosi vilivyoko katika mstari wa mbele Umm Sayala na Jabrat al-Sheikh.
Katika ziara hiyo, Jenerali al-Burhan aliongozana na Gavana wa Darfur Minni Arko Minnawi, Gavana wa Kordofan Kaskazini Abdel Khaliq Abdel Latif na kamanda wa Vikosi vya Sudan Shield Abu Aqla Keikel.
Siku ya Jumapili, jeshi la Sudan lilitangaza kuwa vikosi vyake vimechukua udhibiti wa miji ya Bara, Jabrat al-Sheikh na Umm Sayala kufuatia makabiliano na RSF. Miji miwili iko katika njia ya kimkakati inayounganisha Sudan ya kati na kanda za Kordofan kaskazini na Darfur magharibi.
Majimbo ya Kaskazini, Magharibi na Kusini yamekumbwa na mapigano makali kati ya jeshi la Sudan na RSF tangu Oktoba 2025.
Tangu Aprili 2023, Sudan inashuhudia vita vya ndani vilivyohusisha jeshi na vikosi vya RSF, ambavyo hadi sasa vimeshasababisha vifo vya maelfu ya watu na mamilioni wengine kulazimika kuyahama makazi yao…/