Iran yasambaratisha genge la magendo ya silaha kusini mashariki mwa nchi
Kaimu Kamanda wa Walinzi wa Mpakani wa mkoa wa Sistan na Baluchistan wa kusini mashariki mwa Iran ametangaza habari ya kusambaratishwa genge la magendo ya silaha mkoani humo.
Kwa mujibu wa shirika la habari la IRNA, Kanali Javad Rafiei amesema hayo na kuongeza kuwa, Walinzi wa Mpakani katika kijiji cha Jakigor wako macho saa 24 katika kulinda mipaka ya Iran na wamefanikiwa kukamata silaha na kusambaratisha genge la wafanya magendo ya silaha waliokuwa wanajaribu kutumia eneo hilo kupenyeza silaha haramu ndani ya Iran.
Kanali Rafiei ameongeza kuwa, walinzi hao wa mpakani wamefanikiwa kukamata gari moja lenye silaha na watu wanne waliohusika na magendo hayo.
Tangu baada ya ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamu nchini Iran, madola ya kibeberu yakiongozwa na Marekani na kwa kushirikianana na utawala wa Kizayuni na vibaraka wao hawajawahi kusita hata siku moja kufanya njama za kila namna za kujaribu kuipindua Jamhuri ya Kiislamu ya Iran.
Katika miaka ya hivi karibuni pia, vikwazo vya kiwango cha juu kabisa vya Marekani dhidi ya taifa la Iran vimesambaratishwa. Baada ya kusambaratishwa vikwazo hivyo maadui wameamua kuiwekea Iran vikwazo vikubwa zaidi vya kiusalama. Vikwazo hivyo vinaongozwa na utawala wa Kizayuni wa Israel, Marekani na Uingereza lakini vitasambaratishwa tu kama vilivyosambaratishwa vikwazo na mashinikizo yote ya maadui hao dhidi ya Iran ya Kiislamu.